Katibu wa Habari, Uenezi na Mawasiliano kwa Umma wa Chama cha ACT WAZALENDO Taifa, Salim Biman, leo tarehe 16 Mei 2026 amefungua Mkutano Mkuu wa Kikatiba wa Jimbo la Nungwi uliowahusisha wajumbe zaidi ya 140 kati ya wajumbe 230 wa mkutano huo.

Akitoa nasaha zake kwa wajumbe, Biman alisema mahudhurio hayo yanayoizidi asilimia 59 ni ishara ya uimara wa chama hicho na dhamira yake ya kuendelea kuleta mabadiliko Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

“Hiki ni chama chenye dhamira, siku zote kinaendelea kuwa imara na wanachama wake wako tayari wakati wowote,” alisema Biman.

Mkutano huo pia ulitekeleza matakwa ya kikatiba kwa kufanya uchaguzi wa kujaza nafasi ya Mwenyekiti wa Jimbo, iliyokuwa wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa mwenyekiti wa jimbo hilo.

Kwa upande wake, Naibu Katibu wa Organization, Mafunzo na Uchaguzi Zanzibar wa chama hicho, Khamis Ali Salum, aliwapongeza wajumbe kwa kuitikia na kutekeleza matakwa ya kikatiba ya chama kwa kufanya mkutano huo.

Aidha, ilielezwa kuwa majimbo yote ya Zanzibar ya ACT WAZALENDO yanaendelea na harakati za kufanya mikutano mikuu ya kikatiba ya matawi na majimbo kwa lengo la kuimarisha uhai wa chama.

Katika mkutano huo, mweka hazina wa jimbo alieleza mafanikio yaliyopatikana ndani ya chama licha ya changamoto zilizojitokeza baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.