Na Immaculate Makilika – MAELEZO

Bandari ya Kilwa iliyopo mkoani Lindi imekua ikitumika zaidi kwa shughuli za utalii na kwa kiasi kidogo shughuli za uvuvi.

Kwa kuwa mkakati wa Serikali ni kukuza sekta za uvuvi na utalii nchini, imeanza kutekeleza mradi wake wa kimkakati wa ujenzi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa, sambamba na kusaidia wananchi kunufaika na raslimali za bahari.

Akizungumza leo katika Wilaya ya Kilwa eneo la Kilwa Masoko wakati akiweka jiwe la msingi katika Bandari ya Uvuvi Kilwa na kugawa boti za kisasa 160 kwa wavuvi, ikiwa ni mradi wenye thamani zaidi ya shilingi bilioni 280 Mhe. Rais Samia amesema kuwa Serikali imefanya tukio muhimu la kihistoria kwa kujenga Bandari hiyo ya kwanza ya Uvuvi nchini.

” Boti hizi 160 zimetolea kwa mkopo wa masharti nafuu na unalenga kutoa ajira na kuongeza kipato cha jamii. Boti ndogo zitatumiwa na akina mama kulima mwani na kubeba mizigo, na zile kubwa zinakwenda kwenye kina cha maji
marefu “, ameeleza Rais Samia.

Aidha, Mhe. Rais Samia amesema kuwa Serikali haitarajii boti hizo kuleta ugomvi katika vikundi vya wakulima na wavuvi bali zitumike kuimarisha uchumi wao.

Kwa upande wake, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdallah Ulega amesema kuwa kati ya boti hizo zipo ndogo na zenye ukubwa wa mita14 na uwezo wa kuhifadhi samaki hadi tani moja na nusu.

“Tunakushuru Mhe. Rais kwa kutupa fedha shilingi bilioni 11.5 zitakazowasaidia wavuvi na kazi imeanza. Leo unajenga bandari ya kwanza ya wavuvi, bandari hii inakwenda kuinua uchumi kupitia sekta ya uvuvi kutoka asilimia 1.8 hadi kumi kufikia mwaka 2036, hiyo itawezekana kwa kuwakaribisha wawekezaji wakubwa duniani”, ameeleza Waziri Ulega.

Amefafanua kuwa bandari hiyi itakua na karakana ya meli, sehemu ya kuegesha meli kubwa kumi zenye urefu wa mita30. Aidha, meli kutoka maeneo mbalimbali duniani zitaweza kuweka nanga pamoja na shughuli mbalimbali zitakazofanyika ikiwemo kuongeza chumvi kwenye samaki kabla ya kusafirisha.

Manufaa mengine ya bandari hiyo ni uwezo wa kuhifadhi boti ndogo, sehemu ya kuegesha mitumbwi isiyopungua 200, sehemu ya kuegesha mashua na kutoa fursa ya kutoa ajira kwa vijana takribani 30,000.

“Pia, Bandari hii itakuwa na uwezo wa kuhifadhi samaki tani 1300 kwa wakati mmoja, soko la samaki litakalotumika na wavuvi katika ukanda wa kusini na eneo la kuchakata samaki”, amesisitiza Waziri Ulega.

Aidha, mara baada ya kukamilika kwa ujenzi wa bandari hiyo Mamlaka ya Bandari Tanzania itaendesha shughuli za bandari hiyo kwa kushirikiana na sekta binafsi.

Mnufaika wa mradi huo, Shukrani Shamte ambaye ni mkulima wa mwani ameipongeza Serikali kwa jitihada hizo za Serikali.

“Tunaikushuru Serikali kwa kutupatia mkopo wa boti ya malipo nafuu, boti hizi zitatusaidia kwenye shughuli za kulima mwani kwenye kina cha maji mengi na kubeba mwani kutoka kwenye maji mengi kuja pwani.

“Wakulima wengi wa mwani tunaomba utuwezeshe boti zingine na mahitaji ni mengi na boti ulizotupa ni chache”, ameeleza Bi. Shukrani.

By Jamhuri