Bei za vyakula kuanza kupungua mwezi Machi

Hatimaye Serikali imesema bei ya vyakula itashuka kuanzia Machi ili kuwarahisishia wananchi gharama za maisha.

Hayo yamebainisha na Waziri wa Kilimo Hussein Bashe wakati akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari leo Januari 10, mkoani Dodoma.

Bashe amesema kuwa Serikali imepanga kufungua maghala ya chakula hapa nchini ili kupunguza gharama za vyakula nchini zilizopanda kutokana na ugonjwa Covid 19 pamoja na vita kati ya Ukraine na Urusi.

Bashe amesema wameamua kufanya hivyo kwanza na uzalishaji utakuwa umeongezeka pamoja na kufungua maghala ili kuwanusuru wananchi.

“Tunatarajia kushusha bei ya vyakula kuanzia Machi mwaka huu na ni kutokana na wananchi kulalamika kwa muda mrefu,”amesema Bashe.

Akijibu maswali ya wahariri katika warsha hiyo amesema serikali haitakubali wananchi wake wateseke ili hali chakula kipo katika maghala kimehifadhiwa.

Hata hivyo aliwataka wananchi kutokuwa na wasiwasi kwa sababu serikali imeaikia kilio chao na kuwataka kuwa na subira wakati wakisubiri kushuka kwa bei.

Alifafanua zaidi ya kuwa serikali inakwenda kudhibiti walanguzi ambao nao huchangia kupandisha kwa bei ya vyakula sokoni.

Amesema kuwa serikali imeliona tatizo la kupanda kwa bei ya vyakula sokoni hivyo moja ya mkakati ambao inayo ni kufungua maghala ili kuwarahisishia wananchi katika upatikanaji wa vyakula kwa bei ya vyakula.

Amesema kuanzia Machi hadi Mei mwaka huu chakula kitashuka bei ili kuwarahishia wanachi katika mikoa mbalimbali hapa nchini upatikanaji kwa bei ya kawaida.

Bei ya kilo moja ya unga imefikia kati ya sh.2000 hadi 2500 wakati bei ya kilo moja ya maharage imefikia sh,4000 hadi sh.4500.