Na Mwamvua Mwinyi,JamhuriMedia,Rufiji

Viongozi watatu wa upinzani kutoka Chama Cha Wananchi (CUF) pamoja na ACT Wazalendo pamoja na wafuasi wao 67 wamekimbilia Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Rufiji Mkoani Pwani,huku wakidai Mwenyekiti wa CCM Taifa Samia Suluhu Hassan ni Suluhu ya kero za wananchi kwani anafanya makubwa nchini.

Aidha Jumuiya ya Wazazi wilayani humo imepokea wanachama wapya 600 ambao wameamua kujiunga na Jumuiya hiyo.

Akiwapokea wanachama hao, Mwenyekiti wa wazazi Taifa Fadhil Maganya ameeleza, wanachama hao hawajafanya makosa katika maamuzi yao kwani utekelezaji wa ilani unatekelezwa kwa asilimia kubwa katika nyanja mbalimbali ikiwemo afya kujengwa vituo vya afya, elimu kujengwa madarasa,viwanda na uwekezaji, wawekezaji wanaongezeka nchini, barabara zinaendelezwa kila kona ,vikundi vya ujasiliamali na machinga wanawezeshwa mikopo na miradi mikubwa ya kimkakati haijasimama.

Alihamasisha wapinzani walipo waendelee kuingia CCM na wengine wajiunge kuwa wanachama katika jumuiya za chama hicho.

Maganya ametoa wito kwa watalaam na watendaji wasimamie fedha za miradi na kuhakikisha zinatumika kulingana na wakati ili zilete matokeo chanya.

“CCM ndio jicho pia mhakikishe mnasimamia wataalamu na muendelee kuwafuatilia bila kuchoka”ameeleza Maganya.

Awali Mbunge wa Jimbo la Rufiji, Muhammed Mchengerwa alieleza kazi iliyofanywa na CCM na sasa Samia akiendelea kuifanya Mwenyekiti Samia Suluhu Hassan haijawahi kutokea ,kwani Rufiji za miaka 22 tangu aingie katika siasa sio Rufiji ya sasa.

“Nimeingia kwenye siasa miaka 22 Rufiji ilikuwa kwenye giza katika sekta mbalimbali hasa Nishati ya umeme na miundombinu ya barabara na sasa kero hizo zimebaki historia kutokana na kazi inayofanywa.

“CCM imefanya kazi usiku na mchana,Leo hii ni vijiji vitano pekee ndivyo havina umeme , vingine vyote vina umeme,tumepeleka umeme maeneo yenye hadi km 70, ila bado tunakazi kubwa ya kuendeleza haya,kwa kufanya kazi” amesema Mchengerwa.

Hata hivyo Mchengerwa ameeleza ,tayari viongozi wa Mamlaka ya ujenzi wa barabara,meneja wa Mkoa TANROADS wameshakagua barabara itokayo Chalinze -Utete ,pamoja na hilo Bilioni 46 zimetolewa kukamilisha barabara ya Nyamwage-Utete ambapo mkataba utasainiwa mapema mwezi wa pili mwaka huu.

Mwenyekiti wa CCM Rufiji, Kaswakala Mbonde walieleza ,alieleza viongozi wa upinzani ni watatu ambao wameamua CCM kutoka upinzani,pia wamepokea wafuasi 67 Jumla wakiwa wamepokea wapinzani 70.

Kaswakala alisema, wapo mbio kuwatumikia wananchi Rufiji na kutekeleza ilani ili kuhakikisha maendeleo yanaonekana na kero zilizopo kubaki historia.

Baadhi ya viongozi waliohamia CCM Bashiru Mbukiro almaarufu Bush, alieleza alikuwa ACT Wazalendo , ameona mambo yanaenda vizuri na sasa CCM ipo imara inaupiga mwingi.

“Nipokeeni nimetoka kwa hiari yangu ACT, Mimi nilikuwa kiungo Sasa timu niliyotoka itakuwa imeisha, Mchengerwa umenimaliza tikitiki,!kazi kubwa unafanya,na kwahakika umeuangusha mwamba “ameeleza Bush.

By Jamhuri