KAMATII Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) inakutana leo Jumamosi, Januari 13 ikiwa ni siku nne tangu Edward Lowassa alipofanya ziara Ikulu na kufanya mazungumzo na Rais Dkt. John Magufuli jambo ambalo lilizua mjadala ndani na nje ya chama hicho.

Kikao hicho chini ya Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe, mbali na mambo mengine huenda kitataka kujua undani wa mazungumzo ya Lowassa na Rais Magufuli walipokutana.

Naibu Katibu Mkuu wa Chadema – Zanzibar, Salum Mwalimu jana alitoa taarifa kuwa kikao hicho kimeitishwa kwa lengo la kufanya tathmini ya hali ya kisiasa nchini, ingawa baadhi ya wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema suala la kikao cha Lowassa na Rais Ikulu huenda likawa na mjadala mpana zaidi kwenye kikao hicho.

Mwalimu alisema kikao hicho si cha dharura kwa sababu kilipangwa kufanyika mwezi Desemba mwaka jana na kikaahirishwa kutokana na sikukuu za mwisho wa mwaka.

By Jamhuri