Asema wanaofanya hivyo waache maramoja kwani Serikali imeshashugulikia suala hilo

Ahimiza matumizi ya sayansi na teknolojia katika kuwafundisha watoto

Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia Dar

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila leo Januari 8, 2024 ametoa onyo kwa walimu wakuu wa shule kuacha mara moja tabia ya kuchangisha wanafunzi michango ya madawati na madarasa kwa kuwa Serikali imeshashughulikia miundombinu hiyo

RC Chalamila ameyasema hayo akiwa Oysterbay Sekondari alipofanya ziara ya kutembelea shule za msingi na sekondari kuona uwasili wa wanafunzi ikiwa leo ni siku ya kufungua kwa shule hizo

Hata hivyo Mkuu wa Mkoa ameagiza shule zote zilizopo kwenye “Prime Areas” kujengwa magorofa ili kuweka uwiano Mzuri wa ghorofa lenyewe na eneo lilipo.

Vilevile RC Chalamila amewataka wazazi kuwapeleka watoto wote shule bila ya ubaguzi sambamba na nidhamu kwa watoto kudumishwa kwani watoto ndio Taifa la Kesho

Aidha Mhe. Chalamila ametumia nafasi hiyo kuhimiza matumizi ya “Science na Technology” katika kuwafundisha watoto ambapo amesema kwa sasa waalimu wanafundisha wanafunzi kwa njia ya mtandao

Mwisho kabisa Mkuu wa Mkoa Amehimiza Usafi kuwa Ajenda ya Kudumu kwa wananchi wa Dar es Salaam kwani kwa kufanya hivyo tunaweka Mkoa katika Hali ya Usafi sambamba na kujiepusha na magonjwa mbalimbali Kama vile kipindupindu, homa za matumbo na kuhara hivyo amewataka watendaji na kata kuizingatia Ajenda hiyo.

Kwa upande wa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Saad Mtambule amekiri kupokea maagizo yote na kuahidi kuyafanyia kazi

#Ikumbukwe kuwa Maandalizi yote yameandaliwa vema na wanafunzi hitajika wanaendelea kuripoti mashuleni ishara ya kuonyesha kuwa wazazi wanaridhishwa na miundombinu pamoja na ubora wa elimu inayotolewa

By Jamhuri