ma Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Zanzibar

KATIBU Mkuu Wizara ya Uchukuzi, Prof. Godius Kahyarara ametoa rai kwa Chuo cha Hali ya Hewa Kigoma (NMTC) kuanzisha Shahada ya Sayansi ya Hali ya Hewa (Bsc. in Meteorology) ili kumrahisishia mwanafunzi anayetaka kujiunga katika ngazi ya Stashada (Diploma) kujiendeleza zaidi hadi hatua ya Shahada chuoni hapo.

Aliyasema hayo juzu alipotembelea Banda la TMA lililopo katika maonesho ya Maadhimisho ya Miaka 60 Matukufu ya Mapinduzi ya Zanzibar, yanayofanyika katika viwanja vya Maonesho ya Biashara, Nyamanzi, Mjini Magharibi, Zanzibar kuanzia tarehe 07 – 19 Januari, 2024.

“Kupitia Chuo chenu cha hali ya hewa Kigoma mfanye uwezekano wa kutoa elimu hiyo ya hali ya hewa mpaka ngazi ya degree ili kumrahisishia mwanafunzi anayetaka kujiunga katika ngazi ya Stashada atarajie wepesi wa kujiendeleza zaidi hadi hatua ya Shahada chuoni hapo”. Amesisitiza Prof. Kahyarara

Awali Kaimu Meneja wa Masoko na Uhusiano, Monica Mutoni amefafanua kuwa kwa sasa Stashahada ya sayansi ya hali ya hewa (Bsc. in Meteorology) inatolewa katika chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) pamoja na Stashahada ya Uzamili (PGD). Aidha, aliishukuru serikali kwa uboreshaji mkubwa unaoendelea kufanyika kulingana na mabadiliko ya teknolojia.

Naye Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Zanzibar, ambaye ni Mtaalamu Mwandamizi wa Hali ya Hewa, Hassan Ame ameelezea namna TMA Zanzibar ilivyojipanga katika kuwahudumia wadau wake akisema kwa upande wa Kilimo kuna vituo viwili vinavyowahudumia wadau wa kilimo kimoja kipo Matangatuani, Pemba na kingine Kizimbani, Unguja. Kwa wateja wa bandarini amesema wanahudumiwa na kituo cha Malindi, Unguja pamoja na bandarini Mkoani, Pemba. Katika ufafanuzi wake ameelezea namna TMA inavyoshirikiana na Taasis nyingine ikiwemo Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa (ZDMC), Mamlaka inayohusika na masuala ya usafiri wa Baharini (ZMA) pamoja na Mamlalaka ya Usafiri wa Anga (TCAA).