Na Mwandishi Wetu, JAMHURI MEDIA, Dar es Salaam.

Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Michael Battle amesema serikali inapaswa kutengeneza sekta binafsi imara ili kufikia maendeleo makubwa ya biashara na ujenzi wa viwanda vingi vitakavyoongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira.

Amesema ushirikiano wa muda mrefu wa kibiashara baina ya sekta binafsi ya Marekani na ya Tanzania umekuwa nguzo muhimu katika maendeleo ya biashara na ukuaaji wa uchumi baina ya nchi hizo mbili.

Ameyasema hayo jana wakati mkutano wa US Tanzania Roundtable uliofanyika jijini Dar es Salaam ulioandaliwa na Shirikisho la Wenye Viwanda nchini (CTI) na Shirikisho la Wafanyabiashara wa Marekani Afrika Cooperate Council of Africa (CCA).

Amesema sekta binafsi imara imekuwa msingi mkubwa wa ukuaji wa uchumi kwenye mataifa mengi yaliyoendelea na imekuwa ikisaidia kutengeneza fursa nyingi za ajira zinazosaidia kuwaondoa wananchi kwenye lindi la umaskini na kuwa katika tabaka la kati.

Amesema kama serikali inataka kufikia malengo yake kwa njia nyepesi inapaswa kuendelea kuiwekea mazingira mazuri kuiimarisha sekta binafsi kwani ndiyo yenye uwezo wa kutengeneza fursa nyingi za ajira na kuchangamsha uchumi wa nchi. KuhusuMpango wa Ukuaji na Fursa wa Afrika uliotolewa na Marekani AGOA, Balozi Michael alisema mpango huo umekuwa na manufaa makubwa kwa ukuaji wa uchumi wa mataifa mengi ya Afrika na vyama vyote vikubwa vya Republican na Democrat vimekuwa vikiuunga mkono muda wote.

Amesema hata Rais wa Marekani Joe Biden anaunga mkono mpango huo ambao anaamini utaendelea kutoa mchango mkubwa kwa maendeleo ya nchi za Afrika.

“Rais wa Marekani Jose Biden anaunga mkono AGOA, Bunge la Marekani linaunga mkono mpango huu na bila shaka mnaweza kushuhudia ambavyo umekuwa mkombozi kwa bidhaa za nchi nyingi kuingia kwenye soko la Marekani,” alisema Balozi.

“Mjadala huu wa unaonyesha namna nchi zote mbili zinavyojali uhusiano wa kibiashara kwasababu kuna fursa nyingi za kibiashara baina yetu na tuna wajibu wa kuendeleza uhusiano huu kwa maslahi ya watu wetu,” alisema

Mwenyekiti wa (CTI), Paul Makanza alisema CTI imekuwa na ushirikiano wa siku nyingi na  Shirikisho la Wafanyabiashara wa Marekani kwa lengo la kukuza biashara na uhusiano kati ya Marekani na Tanzania.

Amesema mkutano huo umejadili namna ambavyo wenye viwanda nchini wanaweza kupenya kwenye soko la Marekani na wafanyabiashara wa Marekani wanavyoweza kutumia fursa ya soko la bidhaa mbalimbali nchini Tanzania.

“Tumejadiliana namna ambavyo bidhaa za Marekani zinaweza kuja kirahisi kwenye soko la Tanzania na namna wafanyabiashara wa Marekani wanavyoweza kuja kuwekeza kwenye kutengeneza bidhaa zao hapahapa nchini kwa kuziongezea thamani,” amesema

Alisema bado Tanzania haijalitumia vyema soko kubwa la Marekani kwani imekua ikipeleka malighafi nyingi hasa mazao ya kilimo na madini mbalimbali badala ya kupeleka bidhaa zilizoongezewa thamani.

“Hatupaswi kupeleka malighafi nchini Marekani na tumejadili fursa zilizopo kwenye mpango wa AGOA kwa sasa kuna kampuni kama mbili tu zinapeleka nguo kwenye soko hili kwa hiyo tumejadili namna ya kuongeza ushiriki wa wafanyabaishara,” amesema

Mkurugenzi Mkuu wa (CTI), Leodegar Tenga alisema mkutano ulikwenda vizuri na wameazimia kuendeleza ushirikiano uliopo kwa kuwa karibu na kufahamu wafanyabiashara wa Marekani wana kitu gani na wenzao wa Tanzania wana nini.

“Soko la Marekani ni kubwa mno, nisisi tu ambao tunaweza kutumia hiyo nafasi kukuza uchumi wetu na jana wamarekani walituambia kwamba chini ya mpango wa AGOA bado hatujanufaika sana na nchi zote za Afrika chini ya mpango huu tunauza Dola $ 4 milioni tu kwa mwaka wakati Bangladesh peke yake inauza Marekani Dola milioni 38 kwa mwaka,” alisema

Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Dk. Elsie Kanza, alisema kuna umuhimu wa kuwapa wafanyabiashara taarifa kuhusu bidhaa zinazotakiwa nchini Marekani na kuzitengeneza kwa kuzingatia viwango vitakavyokubaliwa kwenye soko hilo.

“Soko la Marekani ni kubwa sana lakini wafanyabaishara wengi wanashindwa kufikia viwango vinavyotakiwa na siyo tu Tanzania wafanyabiashara wa nchi nyingi za Afrika wamekuwa wakishindwa kuvifikia,” amesema

Balozi alisema katika mkutano maalum wa AGOA uliofanyika kwa siku nne nchini Afrika Kusini wamekubaliana kuwawezesha wafanyabiashara wa mataifa ya Afrika ili waweze kufikia viwango vinavyotakiwa ili waweze kunufaika na fursa ya soko hilo.

“Kwenye mkutano huu tumezungumza sana na kupokea hoja za sekta binafsi ya Marekani na sekta binafsi ya Tanzania ili kuhakikisha tunashirikinana kukuza mauzo ya Tanzania kwenda Marekani na mauzo ya  Marekani kuja Tanzania,” amesema

By Jamhuri