Na Byarugaba Innocent, JamhuriMedia, Kibaha

Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson Simon John amekemea vikali suala la wafanyabishara kuuza vyakula hasa vilivyopikwa kwenye mazingira machafu alipowaongoza wananchi wa Kibaha kufanya zoezi la maadhimisho ya usafishaji mwishoni mwa wiki kwenye soko la mnarani lililopo kwenye Halmashauri ya Mji Kibaha.

Akiwa kwenye harakati za kufyeka nyasi kwenye Soko hilo,Simon alibaini mtaro mchafu na harufu Kali uliokuwa ukitiririsha maji kutoka kwenye banda la mama na baba lishe hali iliyomfanya kukutana na watoa huduma hao ili kujua sababu ili hali wakitambua kuwa kufanya biashara kwenye mazingira machafu ni kuhatarisha afya za walaji.

Mkuu wa Kitengo cha usimamizi wa taka na usafi wa Mazingira Ali Hatibu amemweleza Mhe.Simon kuwa pamoja na kutoa Elimu ya usafishaji na uchambuzi wa taka ngumu na Maji kwa wafanyabiashara hao,bado utekelezaji wake umegonga mwamba.

Mwenyekiti wa mama na baba lishe Saida Hassan amekiri kuwepo kwa changamoto ya Uchafuzi wa Mazingira kwenye eneo lao na kuahidi kuwa Sasa wanakwenda kujiwekea utaratibu utakaomwondoa mfanyabiashara yeyote ambaye hatakuwa na utaratibu wa kufanya usafi na kutunza taka kwenye vyombo maalum kabla ya kusisafirisha kwenda dampo.

Simon ametoa rai kwa wafanyabiashara wote ndani ya Halmashauri ya Mji Kibaha kuhakikisha maeneo yao ya kufanyia biashara ni safi ili kulinda afya za walaji hasa kipindi hiki kinachotabiriwa kuwa na mvua za Elnino.

“Mkurugenzi boresheni Sheria ndogondogo hasa faini za ukusanyaji taka,uzoaji,ulipiaji na upelekaji dampo ili kuendana na wakati wa Sasa na kuimarisha misingi ya usafishaji Mazingira” amesema Simon na kuongeza.

Mamia ya wananchi wakiwemo Makada wa Chama cha Mapinduzi, vyama vya upinzani, Wakuu wa Idara na Vitengo wamejitokeza kwa wingi kuungana na wenzao Duniani kuadhimisha siku ya usafishaji ambayo huadhimishwa kila Septemba,16.

By Jamhuri