Donald Trump na Vladmir Putin Kukutana Leo

 

Rais wa Marekani Donald Trump na wa Urusi Vladmir Putin muda mchache ujao watakutana kwa mazungumzo, katika makazi ya Rais wa nchi hiyo mjini Helsinki, ambao ni mkutano wao wa kwanza kabisa kuwakutanisha pamoja.

Mpaka sasa hakuna ajenda yoyote ya mkutano huo, ambao utahudhuriwa tu na watafsiri wao.

Aidha licha ya mkutano huo kutotegemewa sana, lakini wanaweza kuonesha dalili mpya za kuanza kwa awamu mpya ya mahusiano kati ya Washngton na Moscow, baada ya kufarakana kufuatia Urusi kuitwaa kwa nguvu Crimea.

Aidha wachunguzi wa mambo wanadhani pia kuna hatua inaweza kupigwa katika kuumaliza mzozo wa Syria na pia mazungumzo kuhusiana na masuala ya Nyuklia.

Mkutano huo unaosubiriwa kwa hamu, unakuja baada ya Warusi 12 kushtakiwa kwa makosa ya kufanya uhalifu wa kimtandao wakati wa uchaguzi wa Marekani wa mwaka 2016.

Awali Rais Trump alisema atalizungumzia suala hilo kwenye mkutano huo, licha ya kwamba mkutano huo hauna ajenda maalumu.

Katika hatua nyingine, Viongozi wakuu wa chama cha upinzani nchini Marekani, Democrat akiwemo mwenyekiti wa chama Tom Perez amemtaka Trump kuachana na mazungumzo hayo akidai kuwa Putin ”si rafiki wa nchi yao”.

Kwa upande wa Republican, Seneta John Mccain amesema mkutano ”usiendelee” isipokuwa tu kama Rais ”amejiandaa kumuwajibisha Putin”.