Serikali ya Haiti imetangaza hali ya hatari na amri ya kutotoka nje usiku.

Watu hawataruhusiwa kutoka nje kuanzia saa kumi na mbili jioni hadi saa 11 alfajiri ili kurejesha udhibiti wa nchi baada ya gereza kuu kuvamiwa na genge la wahalifu waliowawezesha maelfu ya wafungwa kutoroka.

Wafungwa 100 tu kati ya 3,800 bado walibaki ndani ya jela hiyo baada ya genge hilo kufanya mashambulizi. Kwa mujibu wa taarifa, watu kadhaa walikufa wakati gereza hilo kuu lililpovamiwa kwenye mji mkuu, Port-au-Prince

Shambulio hilo linafuatia mengine ya hivi karibuni katika mji huo mkuu wa Haiti, ambapo magenge yenye silaha yanayodhibiti sehemu kubwa ya mji huo yamesababisha madhara makubwa tangu wiki iliyopita.

Magenge hayo yanataka kumuondoa madarakani Waziri Mkuu Ariel Henry anayeiongoza Haiti, iliyotumbukia kwenye mgogoro tangu kuuawa kwa Rais Jovenel Moise mwaka 2021.

By Jamhuri