Jacob Zuma Ashinikizwa Kung’atuka Madarakani

Jacob Zuma

Rais wa Afrika kusini anakabiliwa na shinikizo zaidi kujiuzulu kufuatia mazungumzo na maafisa wa ngazi ya juu katika chama chake cha ANC sikuya Jumapili.

Haijafichuliwa mazungumzo hayo yalihusu nini lakini viongozi katika chama hicho wanatarajiwa kufanya mkutano wa dharura hii leo Jumatatu.

Cyril Ramaphosa aliichukuwa nafasi ya kiongozi wa chama cha ANC kutoka kwa Zuma, anayekabiliwa na tuhuma za rushwa.

Wachambuzi wanasema wakuu wa chama hicho wanajaribu kuondoa mvutano wa kung’ang’ania madaraka ambao unaweza kukigawanya chama hicho kabla ya uchaguzi mkuu mwakani.

Wanatarajiwa kuanza mchakato wa kumuondoa rais Zuma kupitia mfumo rasmi wa kumuondoa au kwa kuidhinisha hoja bungeni.

Maafisa sita wakuu wa chama hicho tawala waliwasili mmoja baada ya mwingine Jumapili katika makaaziya Zuma mjini Pretoria.

Walinyamaza kimya wakati mazungumzo yalipomalizika lakini wameitisha mkutano wa kamati kuu ya chama hicho Jumatatu.

Julius Malema, kiongozi wa upinzani na aliyekuwa mafuasi wa chama hicho cha ANC alisema kwenye mtandao wake wa Twitter kwamba rais Zuma amekataa kujiuzulu.

Zuma anastahili kusalia madarakani hadi uchaguzi mwaka ujao 2019. Hatahivyo chama hicho kimepoteza umaarufu wake katika muhula wa pili wa kiongozi huyo huku kukishuhudiwa pia kudorora kwa uchumi na tuhuma za rushwa.

Haki miliki ya picha AFP
Image caption Kiongozi mpya wa chama cha ANC – Ramaphosa, ameshutumu wazi rushwa katika kiwango cha juu, ndani ya chama na pia serikali

Mustakabali wa Zuma ni upi?

Rais Zuma anakabiliwa na tuhuma za rushwa na jitihada za wapinzani na baadhi ya wafuasi wa ANC wanaotaka kumtimua madarakani.

Kwa mujibu wa taarifa rasmi, maafisa wa ngazi ya juu wa ANC wana ‘jadiliana tu’ na rais Zuma kuhusu “ugavi wa uongozi” ndani ya chama.

Lakini nyuma ya kauli hiyo nyepesi – vita vikali vya uongozi vinajitokeza katika nchi hiyo.

Rais Zuma bado yupo madarakani, lakini tangu Desemba mwaka jana, yeye sio mkuu tena wa ANC.

Waendesha mashtaka wakakamavu sasa wanaonekana kushika kasi katika uchunguzi dhidi ya tuhuma za rushwa zinazomkabili bwana Zuma na baadhi ya marafaiki zake wa karibu.

Wengi ndani ya ANC wanamtaka rais huyo ajiuzulu haraka iwezekanavyo, ili waweze kulenga kujenga upya sifa ya chama hicho kufuatia kuwadia kwa uchaguzi mkuu nchini mwakani.

Lakini kuna taarifa kwamba Zuma anajikita kisawasawa.

Anatarajiwa kulihotubia bunge wiki ijayo, lakini wafuasi wa upinzani wanataka kumzuia pia, wakieleza kuwa hastahili kusalia kama rais.

Kiongozi mpya wa ANC, Cyril Ramaphosa, ameshutumu wazi rushwa katika kiwango cha juu ndani ya chama na serikali, lakini anasisitiza kuwa rais Zuma hastahili kuazirishwa.