Jaji Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema mabadiliko katika katiba ya nchi, mfumo wa mahakama, mahakama ya kadhi uliopo leo umetokana na jitihada za Hayati Ali Hassan Mwinyi.

Amesema pia Hayati Mzee Mwinyi  atakumbukwa katika utawala wa sheria kwa kuwa sheria nyingi zilitungwa katika kipindi  chake kifupi alichokuwa Rais wa  Zanzibar.

Jaji Mkuu ameyasema hayo leo Machi 2, 2024 kwenye Uwanja wa Amani Zanzaibar wakati  akitoa salamu za mahakama katika msiba wa Hayati Rais Ali Hassan Mwinyi ambae anazikwa leo kijijini kwao Mangapwani visiwani Zanzibar.

Amesema Tanzania itakapofikisha miaka 100 basi wataandika kitabu ambacho Mzee Mwinyi atachukua nafasi kubwa katika historia .

Amesema, mambo matatu makubwa ambayo sekta ya mahakama itamkumbuka ni  utawala wa sheria, kuchukia rushwa na ustawi wa maendelelo ya watanzania.

“Na hili nimekutana na kumbukumbu ya Machi 8, 1987 alisafiri hadi China, kama mnavyojua China ni nchi ya mfano iliyotoka katika dunia ya tatu na inayokwenda kwa kasi dunia ya kwanza, alikwenda pale akazungumza na kiongozi wa maboresho   Deng Xio Ping nae akamueleza mambo gani ya kuyafanya kama anataka Tanzania itoke kwa haraka kutoka dunia ya tatu kwenda dunia ya kwanza.

“Aliambiwa China inafanya mambo mawili makubwa kitu cha kwanza ni kubadilisha hali ya wananchi wa kawaida, ni jambo alilisimamia sana, alimwambia China kwa muda miaka 30 hadi 50 watajaribu kufanya nchi yao kulingana na nchi ya kwanza hayo ni mambo ambayo  yalimfanya |Mzee Mwinyi afungue soko huria na kuruhusu kila kitu na hapo ndio ukaja usemi wa ‘Mzee Ruksa’

Lakini akaambiwa sharti la kwanza ili nchi ipige  hatua lazima  kuwe na amani duniani, mabadiliko unayofanya ndani hayatakuwa na maana kama duniani hakuna amani, pia  utulivu na amani ndani ya nchi yako ukiwa na hivyo vitu viwili utaweza kubadilisha maisha ya watanzania.

“Alikuwa ni mtu wa haki, alichukua hatua ya kujuzulu wakati akiona haki itaonekana kutendeka akiamua kuchukua uamuzi mgumu.

“Lakini cha tatu, katika kitabu chake cha Mzee Ruksa, kuna ukurasa kazungumzia alivyochukia rushwa akasema kulikuwa na semina moja ya haki na kupambana na uhalifu ilifanyika katika Chuo cha Polisi Zanzibar Agosti 6, 84 iliandaliwa na Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na wadau wengine wa sheria, wakati ule kulikuwa na tuhuma nyingi katika Jeshi la Polisi, rushwa na matatizo mengine ya kimaadili na kiutendaji.

“Amesema jambo ambalo nikiwa Rais mpya wa Zanzibar lilinikera sana, siku hiyo nilikuwa na ziara ya kwenda Kigoma niliamua kuifungua semina hiyo mimi mwenyewe  baadhi ya mambo niliyosema kwa nguvu na msisitizo, haki itendeke, ionekane kuwa imetendeka kwa wakati bila ucheleweshaji husio na lazima.

“Sura ya Mahakama kama Polisi na waendesha mashitaka inaharibiwa na wachache wanaopindisha sheria na taratibu, kutokana na uzembe, rushwa na upendeleo, mahakama ni mhimili huru wa serikali, lazima wajue wao ni sehemu ya jamii na wanao wajibu wa kurekebisha kasoro katika jamii,  ikiwemo uhalifu na kusimamia haki kuhakikisha kwamba makosa yanaadhibitiwa  mara moja;

“Na wale wasiokuwa na hatia wanaachiwa mara moja, niliwakumbusha mahakama na sekta ya sheria inatakiwa kuwa na heshima mbele ya jamii  kwa vitendo vyake,  na kwa vile  upapambanaji wa utoaji haki unahitaji ushirikiano niliwasihi umuhimu wa ushirikiano,”Jaji Mkuu alinukuu maneno yaliyopo katika kurusa mojawapo ya kitabu cha Mzee Mwinyi.

By Jamhuri