Je, unamfahamu mnyama duma (Cheetah)? Wengi  wanajua tu kwamba ni kati ya wanyama  wenye kasi sana. 

Duma anakimbia zaidi ya maili 60 kwa saa, lakini wengi wasichokijua kuhusu mnyama huyu ni uwezo wake mkubwa wa kubadili uelekeo  kinyume na alikokuwa anakimbilia kwa kasi ile ile aliyokuwa nayo. Hapa amewashinda wanyama  wengine wote.

Wengi wetu tuna kasi sana ya maisha, kasi ya  kutafuta ajira, kasi ya mahusiano, kasi ya kutafuta  elimu nzuri, kasi ya kuzisaka fursa na kwingineko kwingi. Swali ni: Je, endapo kunatokea  mabadiliko ya ghafla kwenye eneo fulani maishani mwako, una uwezo kiasi gani wa kubadili kasi yako ili uendelee kukimbia kwenye uelekeo mwingine? 

Au ndiyo uelekeo ukibadilika na wewe unalala chali na kuanza kulalamika? Amua kubadilika.  Kila asubuhi jiambie: “Nataka kuwa kama duma.”

Kila asubuhi unapoamka, amka na wazo jipya.  Kila asubuhi weka malengo kwenye vipaumbele  vyako. 

“Kila  asubuhi ninaisikia sauti ya ushindi ndani  ya akili yangu.  Na moyo wangu unaniambia: Utafanikiwa” aliandika  mtu  fulani. 

Jifunze jambo kutoka kwa Jessica Cox. Jessica  Cox ni rubani mwanamke asiye na mikono.  Jessica  Cox ni mwanamke Mmarekani  aliyezaliwa mwaka 1983 bila mikono, lakini ndiye  mwanamke wa kwanza duniani kupata leseni ya  kurusha ndege. 

Huyu ni mwanamke anayeongoza ndege kwa  kutumia miguu yake. Jessica Cox katika kitabu  chake cha  “Disarm Your Limits”  anasema:  “Kila asubuhi ninaamka nikiwa nimejaa roho ya  ushindi katika maisha yangu.”

Kila asubuhi jiamini kabla hujaaminiwa. Kila  asubuhi jijenge kabla hujajengwa.  Kila asubuhi  jitambue kabla hujatambuliwa. 

Kila asubuhi jipende kabla hujapendwa.  Jessica  Cox  aliamini kwamba anaweza kuwa rubani  licha ya kwamba hana mikono. 

Kila  asubuhi unapoamka vunja minyororo  inayokufanya usijiamini. Kila asubuhi  unapoamka vunja minyororo ya uvivu. Kila  asubuhi unapoamka vunja minyororo ya laana.  Kila asubuhi unapoamka vunja minyororo ya  umaskini.  

Kila  asubuhi  unapoamka vunja minyororo ya  kukawia kufanikiwa.  Kila  asubuhi  unapoamka  vunja minyororo ya kukataliwa na kujikataa.  Kila  asubuhi unapoamka vunja minyororo ya  kutangatanga. Kila asubuhi  unapoamka vunja minyororo ya  sauti  za  kushindwa.  Kila asubuhi unapoamka vunja  minyororo ya hofu.

Maisha ya mafanikio duniani ni haki ya kila mwanadamu. Hakuna binadamu aliyeletwa  duniani kuja kushuhudia watu wengine wakifanikiwa huku yeye akiwa anakumbatiwa na  umaskini. 

Kila mtu ana fungu lake. Kila mwanadamu mwenye pumzi anayo haki, nafasi, uwezo na uchaguzi wa kufanikiwa.

Ahadi ina nguvu. Ahadi ni muujiza. Kila asubuhi  jitahidi kufanya jambo fulani. Jiahidi kwamba  utafanikiwa. Jiahidi kwamba utakuwa mtakatifu.  Jiahidi kwamba utakuwa mfanyabiashara  mkubwa.  Jiahidi kwamba utakuwa mwanandoa  mwaminifu. 

Jiahidi kwamba utakuwa mtii kwa Muumba wako. Jiahidi kwamba utakuwa kiongozi bora.  Jiahidi  kwamba utakuwa bilionea.  Amini! Amini! Amini!

Kila asubuhi amka na moyo wa uthubutu.  Mhamasishaji, Les Brown anasema: “Ili uwe mtu  ambaye haujawahi kuwa ni  lazima ufanye  mambo ambayo hujawahi  kufanya.” 

Woga hauna mtaji lakini uthubutu una mtaji.  Ukiogopa hauwezi kufanya chochote, lakini  ukithubutu utafanya chochote.  Kuna muujiza  mkubwa umejificha ndani ya kile unachoogopa  kukifanya.

Kila  asubuhi, piga hatua. Mwandishi wa insha na  mashairi wa Marekani, Ralpha Waldo Emerson  anasema: “Maisha ni hatua, si kituo.”  Maisha  yana thamani kama unapiga hatua. Umri wako  wa kutambaa umepita.  Piga hatua.

Kila asubuhi jiulize maswali.  Jiulize maswali  ya  mafanikio.  Unapotaka  kufanikiwa usiogope  kuuliza maswali.  

Maswali ni nusu ya majibu. Unapojiuliza swali unakuwa uko karibu kupata jibu la swali unalojiuliza. 

Mjasiriamali na mtunzi wa vitabu,  Robert  Kiyosaki, anasema: “Watu waliofanikiwa sana  katika maisha ni wale ambao huuliza maswali. Kila mara wanajifunza. Kila mara wanakua. Kila mara wanasukuma mambo.”  Unapojiuliza huwa  unataka kupata majibu.  Mwandishi  wa  Marekani,  Tony Robbins, anasema: “Watu  waliofanikiwa wanauliza maswali zaidi na  matokeo yake wanapata majibu mazuri zaidi.”

Kila asubuhi uliza maswali na jiulize maswali.

By Jamhuri