Na Helena Magabe, JamhurMexia, Tarime

Mjumbe wa Kamati kuu ya CHADEMA John Heche ambaye pia amewahi kuwa Mbunge wa Tarime Vijijini jana amehojiwa Polisi na kutaja orodha ya watu waliotekwa na kupotea.

Akizungumza kwa njia ya simu na Jamhuri kuhusu kuitwa Polisi na kuhojiwa jana juu ya tuhumu Jeshi la Polisi kumteka mwananchi wa Serengeti amekiri kuwa ni kweli amehojiwa na kumtaja mtu huyo majina yake ambaye ni Charles Chacha Weitinyi.

Amesema si huyo tu aliyepotea mikononi mwa Polisi bali amewataja na wengine zaidi ya 10 kwa majina yao katika ofisi hizo za RPC Mkoa alipokuwa akihojiwa na RCO.

“Nimehojiwa nikawapa na majina ya watu wengine zaidi ya 10 walichukuliwa kama huyo na kutoweka wengine ni kwenye hifadhi na wengine ni mgodini na hata wengine wamepoteza maisha majina hata majina yao nimewatajia” amesema John.

Amefafanua kuwa kuanzia kipindi cha Septemba 2023 hadi sasa zaidi ya watu saba wameuwawa na wengine saba wamepoteza maisha katika mazingira ya kutatanisha jeshi likidaiwa kuhusika.

Akiendelea kuzungumza amesema kuwa aliandika juu ya tukio hilo mtandaoni ili RPC afuatilie juu ya tukio hilo na mtu la Charles Chacha Weitinyi kwa sababu ni wajibu wake kufanya kufatilia.

Amefafanua kuwa Oktoba 22,2023 Weitinyi alifikishwa kituo cha Polisi Mugumu Serengeti kuna watu waliomuona kituoni hapo na pikipiki yake lakini hakurudi nyumbani.

Aidha amesema kesho yake Oktoba 23,2023 familia yake ililazimika kufatilia katika kituo hicho na kuambiwa hayupo na ile pikipiki haikuwepo.

” Ni lazima tufatilie maana haiwezekani mtu mzima mwenye miaka zaidi ya 30 apotee hivi hivi kuna mtu alikuwa pale kituoni kwa mambo yake alimwona na wengine walimwona baadae pikipiki haikuoneka ” amesema John.

Hata hivyo Heche ambaye ametinga Kituo cha Polisi na Mawakili waliwili amesema RCO amepokea taarifa yake na ameahidi kuifanyia uchunguzi.

Alipohojiwa kwa nini atinge na makili wawili amesema ni kawaida ukiitwa Polisi ni lazima uende na wadhami au mawakili wako.

Kwa upande wa Jeshi la Polisi Jamuhuri imejitahidi kupiga namba za Ofisi ya RPC Mkoa ili Kamanda Salumu Marcase ajibu tuhuma hizo lakini namba hizo hazikuweza kupatikana hewani.

By Jamhuri