Kamati ya mawaziri yajionea uvamizi kwenye chanzo cha maji Katavi

Na Munir Shemweta,JamhuriMedia,Katavi

Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta imetembelea maeneo ya hifadhi na chanzo cha maji katika mkoa wa Katavi kujionea hali ya uvamizi wa maeneo hayo na kuelekeza wananchi waliovamia maeneo hayo kutofanya maendelezo mpaka hapo timu ya wataalamu itakapokamilisha kazi yake kuhusiana na mgogoro wa matumizi ya ardhi kwenye maeneo hayo.

Kamati hiyo inayohusisha Wizara nane za kisekta Oktoba 12, 2022 ilitembelea eneo la hifadhi la mito miwili lilipo kitongoji cha Kasekese wilayani Tanganyika pamoja na chanzo cha maji cha Milala kilichopo kata ya Misunkumilo manispaa ya Mpanda mkoani Katavi.

Kiongozi wa Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta Mashimba Ndaki (Kulia) akizungumza na Naibu Waziri Maliasili na Utalii Mary Masanja wakati wakitoka kutembelea eneo la hifadhi la Kasekese wilayani Tanganyika mkoa wa Katavi 

Kiongozi wa Kamati ya Mawaziri wa Kisekta katika ziara hiyo Mhe. Mashimba Ndaki aliwaeleza wananchi wa Kisekese kuwa, uamuzi wa mwisho kama eneo hilo liendelee kuwa hiadhi au maeneo ya kuishi watu itajulikana baada ya kupata majibu kutoka kwa wataalamu.

‘’Ndugu wananchi naomba mnielwe eneo hili mnalolikalia halijaeleweka kama ni makazi yenu na vizuri tuelewe ingawa ukweli wenyewe mgumu lakini ni vizuri kuelewa kwa sababu lina sura mbili ni eneo la hifadhi au kupita wanyama lakini ninyi mpo mmekaa’’ alisema Ndaki.

Aliwataka wananchi hao kuwa wavumilivu wakati wataalamu wanafanyia kazi suala hilo na kamati yake ikishapa majibu kuhusiana na suala hilo basi uamuzi kamili wataelezwa kati ya mambo mawili ambayo ni ama eneo hilo ni hifadhi au eneo la kupita wanyama.

Baadhi ya wananchi wa Kasekese wilayani Tanganyika mkoa wa Katavi wakifuatilia maelezo ya Kamati ya Mawaziri wa Wizara za Kisekta ilipotembelea eneo hilo 

Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Ridhiwani Kikwete aliwaeleza wananchi wa Kasekese katika mkutano wa hadhara kuwa, kwa mujibu wa sheria za ugawaji ardhi hakuna mahali popote panaposema kuwa kiongozi anaweza kugawa ardhi kwa wananchi.

‘’Sheria hizi zote mbili nilizozitaja hakuna hata sheria moja iliyompa mamlaka mkuu wa wilaya au mkuu wa mkoa kugawa ardhi na ndiyo maana nimestuka sana niliposikia kuwa kuna mkuu wa wilaya amewachukua watu na kwenda kuwagawia ardhi, huyo mkuu wa wilaya amewaingiza chaka’’ alisema Ridhiwani.

Mawaziri wa Wizara za Kisekta wakipata maelezo ya uvamizi wa eneo la hifadhi la mito miwili eneo la Kasekese kwa Mkuu wa Wilaya ya Tanganyika mkoa wa Katavi Onesmo Busweru (kushoto) wakati Kamati ya Mawaziri hao ilipotembelea eneo hilo kujionea hali halisi

Akigeukia suala la chanzo cha maji cha Milala kilichopo Manispaa ya Mpanda, Waziri Ndaki aliwaambia wananchi wanaoishi eneo hilo kuwa, taarifa za awali zinaonesha kuwa wananchi hao wamevamia chanzo hicho na wanatakiwa kuondoka. Hata hivyo, alibainisha kuwa, uamuzi wa mwisho wa aidha kubaki ama kuondoka eneo hilo utaamuliwa pale Kamati yake itakapopata ushauri kutoka serikali ya mkoa wa Rukwa.

Kamati ya Mawaziri nane wa Wizara za Kisekta iliyoanza kazi kwenye mkoa wa Rukwa imemaliza ziara yake mkoani Katavi na inaendelea na ziara hiyo katika mkoa wa Kigoma na baadaye Kagera.