Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi David Kihenzile akitoa maelekezo kwa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) wakati alipotembelea karakana ya ndege inayomilikiwa na Shirika hilo iliyopo katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro Mkoani Kilimanjaro.

Serikali imesema uwepo wa Karakana ya Matengenezo ya Ndege inayomilikiwa na Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) kumepunguza gharama za matengenezo kwa zaidi ya asilimia hamsini hali inayosaidia Kampuni hii kutumia fedha hizo kwenye maeneo mengine.

Akizungumza wakati alipotembelea Karakana hiyo iliyopo katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi David Kihenzile amesema maboresho mbalimbali yaliyofanywa kwa ATCL yana lengo la kufanya Kampuni hii kujiendesha kwa faida.

“Karakana hii imeleta ahueni kubwa kwa ATCL na Serikali sababu fedha zinazookolewa kwa kufanya matangenezo ndani ya nchi yameiwezesha Kampuni hii kupiga hatua kwani fedha hizo hizo zingeweza kwenda nje ya nchi na kunufaisha nchi zenye makampuni hayo, hongereni sana, amesema Naibu Waziri Kihenzile.

Naibu Waziri Kihenzile pia amempongeza Mkurugenzi Mkuu wa ATCL Mhandisi Ladislaus Matindi kwa kuhakikisha kuna utaratibu mzuri wa kutumia watalaam wa Kampuni hii katika matengenezo makubwa na madogo kipitia Karakana hiyo.

Aidha, Naibu Waziri amemtaka Mkurugenzi Mtendaji Mhandisi Matindi kuhakikisha anaboresha eneo la huduma kwa wateja ili kuvutia wateja wengi zaidi kushawishika kutumia Kampuni hii kwa safari zao za ndani na nje ya nchi.

Naye Mkurugenzi Mtendaji Mhandisi Matindi amesema kwa sasa ATCL imejipanga kuongeza vyanzo vya mapato kwa kuwa na Karakana yenye wataalam wenye leseni za kufanya matengenezo makubwa ya ndege hadi kiwango cha Check – C  na kuanzisha sehemu maalum za mapumziko (Twiga Lounge) kwa abiria wanaosafiri nje ya nchi.

Pia Mha. Matindi ameahidi kuendelea kutatua changamoto zinazowakabili ili kushindana zaidi kimataifa.

Serikali imetoa takribani bilioni 20 kwa kutekeleza mradi wa maboresho ya Karakana hiyo pamoja na nyumba zaidi ya 30 za Kampuni hiyo zilizoko mkoani Kilimanjaro.

Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi David Kihenzile akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) Mhandisi Ladislaus Matindi kuhusu hatua mbalimbali za matengenezo ya ndege katika karakana ya ndege linalomilikiwa na Shirika hilo iliyopo Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro Mkoani Kilimanjaro.

Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi David Kihenzile akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) Mhandisi Ladislaus Matindi kuhusu hatua iliyofikiwa ya matengenezo ya Ndege aina ya A220-300 yanayofanywa katika karakana ya ndege inayomilikiwa na Shirika hilo iliyopo katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro Mkoani Kilimanjaro.
Naibu Waziri wa Wizara ya Uchukuzi David Kihenzile akimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) Mhandisi Ladislaus Matindi kuhusu mipango mbalimbali iliyopangwa na shirika hilo kwa matumizi ya karakana ya ndege inayomilikiwa na Shirika hilo iliyopo Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro Mkoani Kilimanjaro.

By Jamhuri