KAULI ZA WASOMAJI

Daraja la Mbutu vipi?

Pongezi kwenu waandishi wa Gazeti JAMHURI kwa kutujulisha habari zenye weledi. Kero yangu ni ujenzi wa daraja la Mbutu. Kasi ya ujenzi wa daraja hili umekuwa wa kusuasua, na masika karibu yanaanza. Jamani mnaohusika na ujenzi huu fanyeni haraka kuukamilisha kuepusha wananchi kusombwa na maji wakati wa mvua za masika.

 

Michael Hengele, Igunga

0755 217 329

 

 

Bomoabomoa itaisha lini?

Hivi hiyo bomoabomoa ambayo sasa inaonekana kuwa kama maisha, hasa katika Jiji la Dar es Salaam itaisha lini jamani? Hivi viongozi wa Serikali mlikuwa wapi mpaka wananchi wanajenga mahali pasiporuhusiwa? Ifike mahali Watanzania wajivunie nchi yao badala ya kuvumilia kuwa katika nchi yao.

 

Maheri Maheri, Bukoba

0785 880 350

 

 

Big Results Now mh!

Eti Big Results Now (BRN) katika elimu! Bila kumung’unya maneno- BRN; usimamizi wa idara za sekondari na ualimu ukiendelea kuwa chini ya TAMISEMI iliyojaa ubabaishaji tutarajie anguko kubwa hapa nchini mithili ya MNARA WA BABELI. Cha msingi Serikali irudishe usimamizi wa elimu kwa walimu wenyewe.

 

Msomaji wa JAMHURI, Singida

0782 566 681

 

 

Serikali ianzishe, UVT, UWT

Ili kujenga taifa lenye utaifa, ninashauri Serikali iunde makundi yafuatayo yawe ya utafiti, yasiwe ya vyama vya siasa: Umoja wa Vijana Tanzania (UVT) na Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT). Hatua hiyo itajenga uzalendo, umoja, mshikamano na utaifa wa kujenga taifa imara na lenye nguvu imara.

 

H. J. Msengi, Morogoro

0784 249 355


 

Tusibague wahamiaji haramu

Hivi wahamiaji haramu ni Wanyarwanda tu. Mbona naona Wanyasa kibao kule Masaki, Wamakonde wa Msumbiji kule Msasani, Wakongo kule Kinondoni, Wahindi kule Upanga, jijini Dar es Salaam? Au kuna watu wanalengwa kwa sababu ni wafugaji wazuri kuliko sisi?  Si kila mtu anayeishi Roma ni Mkatoliki.

Pius Bwanakunu, Karagwe

0717 443 737

 

Mansoor hayuko peke yake

Mansoor Himid Yussuf si wa kwanza kuwa mnafiki ndani ya CCM, afadhali amevuliwa uanachama, kwa sababu ndiye aliyetaka kukigeuza chama hicho huku Zanzibar wakati wa uchaguzi uliopita. Inadaiwa alipanga njama na Aman Karume, na ndiye anayetwambia tuwachukie Watanganyika.

Hasan, Zanzibar

0773 379 931

 

 

Lowassa anafaa kuwa rais

Tanzania ijayo itakuwa ya maziwa na asali, itakuwa mithili ya Kaanani mpya endapo Mheshimiwa Edward Lowassa atakubali kugombea urais mwaka 2015. Ni dhahiri ataendeleza mazuri yote atakayoacha Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete. Mungu amzidishie Mheshimiwa Lowassa afya na baraka tele.

 

Msomaji wa JAMHURI

0788 363 891

 

 

Viongozi wanaomchukiza Mungu

Nakerwa sana na viongozi wa dini kujihusisha na mambo yanayomchukiza Mungu kutokana na tamaa ya mali zikiwamo zinazotokana na biashara ya dawa za kulevya na kuwachangisha waumini fedha ngingi kwa nguvu na kutishia kuwafungia huduma za kiroho wasiochanga. Hiyo ni dhambi kubwa kwa Mungu.

 

E. F. Kachira, Dar es Salaam

0652 054 578