Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) itajenga kituo cha umahiri cha kutoa huduma za utengamao kwa wagonjwa wa Afya ya Akili huko Kijiji cha Vikuruti kikichopo Kata ya Chamazi- Manispaa ya Temeke.

Hayo yamesemwa leo Oktoba 19, 2023 na Mkurugenzi Mtendaji wa MNH Prof. Mohamed Janabi katika maadhimisho ya siku ya Afya ya Akili duniani ambayo hufanyika kila mwaka Oktoba 10.

Prof. Janabi amesema MNH ina eneo Vikuruti lenye ukubwa wa hekari zaidi ya 160 hivyo kuna nafasi ya kutosha kujenga kituo hicho cha umahiri kwa ajili ya matibabu ikiwemo wananchi wa kawaida ambao watahitaji muda wa pekee wa kutulia na kufanya tafakari binafsi.

Amesema kituo hicho kitakua na majengo ya kisasa ya kupumzika, mandhari ya kuvutia, miradi mbalimbali ya kimkakati kwa ajili ya kusaidia wahitaji kama sehemu ya Tiba kazi ikiwa ni maandalizi ya kumrudisha kwenye jamii mgonjwa husika.

Amesema takwimu za MNH zinaonesha takribani warahibu wa dawa za kulevya wapatao 1,000 hunywa dawa aina ya Methadone kila siku MNH-Upanga na warahibu zaidi ya 5,000 wamepata huduma hiyo tangu mradi huo uliponzishwa.

Aidha wagonjwa 70 hadi 100 wa Afya ya Akili huonwa kila siku katika Kliniki hizo katika kampasi ya Upanga na Mloganzila.

Prof. Janabi
ametoa Rai kwa wananchi kufahamu na kutofautisha kuwa si kila mgonjwa wa Afya ya Akili ametokana na pombe au dawa za kulevya.

Amesema wengine wanapata changamoto ya Afya ya Akili kutokana na sababu mbalimbali zinazowakabili na kushindwa kuhimili.

Kauli mbiu ya siku ya Afya duniani kwa mwaka huu ni AFYA YA AKILI HAKI YA KILA MTU.