Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam

Wajumbe wa Bodi ya Ushauri ya Wizara ya Afya kwa TMDA (MAB), wamefanya ziara katika viwanda vinavyozalisha bidhaa za dawa na vifaa tiba vilivyoko katika mikoa ya Dar es Salaam na pwani kwa lengo la kujifunza na kujionea namna shughuli za uzalishaji zinavyofanyika ikiwa ni pamoja na kujiridhisha na msaada wa kiufundi unaotolewa na TMDA kwa viwanda.

Ziara hiyo ya viwanda imefanyika kuanzia tarehe 23 – 25 Januari, 2023 ikihusisha Menejimenti ya TMDA inafanyika kufuatia kuteuliwa kwa Bodi mpya ya Wizara ya Afya kwa TMDA baada ya bodi ya awali kumaliza muda wake mnamo Juni 2023.

Mkurugenzi Mkuu wa TMDA, Bw. Adam Fimbo, amesema lengo la ziara hii ya wajumbe wa MAB katika viwanda vinavyozalisha bidhaa za dawa na vifaa tiba ni kuhakikisha wajumbe hao wanapata uelewa wa pamoja wa namna udhibiti wa ubora, usalama na ufanisi wa bidhaa unafanyika kuanzia katika viwanda kabla hazijafika kwa mtumiaji wa mwisho.


Wakizungumza kwa nyakati tofauti, wamiliki wa viwanda vya MANSOORDAYA CHEMICAL LIMITED, ZENUFA LABORATORIES LIMITED, SHELLYS Pharmaceuticals na KAS BIOTECH LTD wamesema kuwa uzalishaji wa bidhaa za dawa na vifaa tiba unafanyika kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali inayotolewa ili kukidhi viwango vya kimataifa lakini pia ili kulinda afya ya jamii.

Aidha, wameieleza bodi kuwa TMDA imekuwa ikitoa ushirikiano na msaada wa kiufundi wa kutosha na tunaomba waendelee hivyo katika kuhakikisha dawa na vifaa tiba vinavyozalishwa vinakidhi matakwa ya sheria nchini na kimataifa.

Naye Mwenyekiti wa Bodi (MAB), Bw. Eric Shitindi, ametoa pongezi nyingi kwa viwanda hivyo kwa kusimamia vizuri uzalishaji wa bidhaa hizo na kuwataka kuendelea kuzingatia ubora, usalama na ufanisi wa bidhaa hizo ili kulinda afya ya jamii, kwani wakifanya vinginevyo kutakuwa na madhara makubwa sana kwa watanzania wanaotumia bidhaa hizo.

By Jamhuri