Mtu mmoja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 60 Idd Abdalah amefarikia dunia kwa kuburuzwa na maji huku Kaya zaidi ya 150 katika Kata ya Mvumi na Ludewa Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro zikikosa makazi baada ya nyumba zao kujaa maji, kufuatia mafuriko yaliyosababishwa na Mto Wami kujaa maji na kupoteza mwelekeo.

Akithibitisha kuwepo kwa athari zilizosababishwa na mafuriko hayo, Mkuu wa Wilaya ya Kilosa Shaka Hamdu Shaka, amesema tayari kumetengwa maeneo maalum kwa wahanga wa mafuriko hayo ambapo kwa upande wa Ludewa, Kamati ya Maafa imetenga Shule ya Mkondo B pamoja na Shule ya Msingi Gongwe kwa Kata ya Mvumi.

Amesema tayari utekelezaji umeenza kufanyika ikiwemo matibabu kwa waliopata majeraha huku akitoa rai kwa wananchi waishio pembezoni mwa mito kuishi kwa tahadhari.