Uongozi wa Bendi mpya ya muziki wa dansi ya Malaika iliyoundwa hivi karibuni, umesema kuwa umeamua kufanya muziki kwa kuzingatia ubunifu, tofauti na zilivyo bendi nyingine za muziki huo ili kukamata soko.

Bendi hiyo makazi yake jijini Dar es Salam inaundwa na wanamuziki maarufu Tanzania — Christian Bella na Toto Ze Bingwa — ambao awali walikuwa wakifanya kazi zao za muziki katika Bendi ya Akudo Impact.

Kabla ya Ze Bingwa kujiunga na Akudo Impact, aliwahi kufanya muziki na kundi la FM Academia la jijini maarufu kama Wazee wa Ngwasuma wakiongozwa na Rais wao, Nyoshi el Sadat ‘Sauti ya Simba’. Meneja wa bendi hiyo, Fadhili Mfate ameiambia JAMHURI kuwa bendi hiyo itazinduliwa Novemba 15 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

 

“Tunatarajia kuingia sokoni kwa nguvu kubwa tukiwa na lengo la kukamata soko kwa kasi, na hii si mchezo hapa saula ni utendaji mzuri tu,” amesema Mfate.

Amesema kuwa kwa sasa kuna bendi nyingi za muziki wa dansi ambazo wanaziona kama wapinzani wao, na hivyo wanatakiwa kuwa na bunifu-mbadala za kuweza kuzipiku bendi hizo.

Bendi ya Malaika imeundwa hivi karibuni  kwa kuwajumuisha wanamuziki maarufu katika muziki wa dansi.

 

Wachambuzi wa mambo ya muziki Tanzania wanasema kuwa bendi hiyo italeta ushindani mkubwa katika tasnia ya muziki wa dansi, kutokana na kuwa na wanamuziki maarufu ambao wana uwezo wa kuvuta hisia za wapenzi wa muziki huo na hasa pale wanapokuwa jukwaani.

 

0783 106 700


By Jamhuri