DAR ES SALAAM

Na Mwandishi Maalumu

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA) iliyo chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imetoa ufafanuzi wa kina kuhusu aina mbalimbali za chanjo za Covid – 19 (corona). 

Ufuatao ni ufafanuzi/majibu ya TMDA kuhusu chanjo za corona. 

1. Chanjo za Covid – 19 ni nini? 

Chanjo za Covid – 19 ni bidhaa za kibaiolojia zilizotengenezwa ili kukinga mwili dhidi ya virusi vya ugonjwa wa homa kali inayoathiri mfumo wa upumuaji aina ya SARS – CoV-2 ambavyo  husababisha  ugonjwa  wa  virusi  vya  corona unaojulikana  kama Covid-19. 

2. Ni aina ngapi za chanjo za Covid-19 na zinafanyaje kazi? 

Chanjo za Covid – 19 zimetengenezwa ili kuufundisha mwili kujikinga, kutambua na kuzuia maradhi yanayosababishwa na virusi vya Covid – 19. Hadi sasa kuna aina kuu nne za chanjo za Covid-19 ambazo zimegundulika na kuanza kutumika duniani: 

 • Chanjo ambazo virusi vya Covid-19 vimeondolewa makali au kudhoofishwa. Hizi hutumia virusi vya corona ambavyo vimedhoofishwa na kutosababisha magonjwa lakini zinaweka kinga kwa mtumiaji. 

• Chanjo zitokanazo na protini. Hizi hutumia vipande  vya protini visivyo na madhara au ganda la protini ambalo hufanana na virusi vya Covid-19 ili kutoa kinga ya mwili. 

• Chanjo za vekta za virusi. Hizi hutumia virusi salama ambavyo haviwezi kusababisha magonjwa lakini hutumika kama sehemu ya kutengenezea protini za virusi vya corona ili kutoa kinga. 

• Chanjo zitokanazo na vinasaba (RNA na DNA). Hizi hutumia RNA au DNA iliyoundwa na vinasaba kutoa protini ambayo husababisha kinga ya mwili.  

3. Kuna chanjo ngapi za Covid-19 zilizoidhinishwa kutumika hadi sasa? 

Kuna chanjo 20 zilizoidhinishwa na angalau mamlaka moja ya udhibiti duniani kwa ajili ya matumizi kama ifuatavyo: 

 • Chanjo mbili za aina itokanayo na vinasaba (RNA) (Pfizer–BioNTech na Moderna). 

• Chanjo tisa za virusi ambavyo vimeondolewa makali au kudhoofishwa  (BBIBP-CorV, Chinese Academy of Medical Sciences, CoronaVac, Covaxin, CoviVac, COVIran Barakat, Minhai-Kangtai, QazVac, and WIBP-CorV).  

• Chanjo tano za aina ya vekta za virusi (Sputnik Light,  Sputnik  V,  Oxford–AstraZeneca, Convidecia na Janssen). 

• Chanjo nne zitokanazo na protini (Abdala, EpiVacCorona, MVC-COV1901, Soberana 02 na ZF2001). 

Kwa ujumla hadi sasa, kuna chanjo 330 ambazo ziko  katika hatua mbalimbali za uvumbuzi ikiwa ni pamoja na 102 zilizo katika hatua ya utafiti, 30 katika majaribio ya awamu ya kwanza, 30 katika majaribio ya awamu ya pili, 25 katika majaribio ya awamu ya tatu na nane katika majaribio ya awamu ya nne. 

4. Aina gani za chanjo zimeorodheshwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa matumizi ya dharura? 

 Hadi sasa WHO limeorodhesha aina nane tofauti za chanjo kwa matumizi ya dharura (EUL) kama ifuatavyo: 

 1.  Pfizer/BioNtech – BNT162b2/COMIRNATY Tozinameran mtengenezaji akiwa ni Pfizer/BioNtech – Marekani/Ujerumani.

2.  Astra Zeneca – AZD1222 mtengenezaji akiwa AstraZeneca –Uingereza. 

3.  Astra Zeneca – AZD1222 mtengenezaji akiwa ni AstraZeneca (MFDS KOREA) – Uingereza na Korea. 

4.  Covishield (ChAdOx1_nCoV-19) mtengenezaji ni Serum Institute of India Pvt. Ltd – India. 

5.  Janssen – Ad26.COV2.S mtengenezaji akiwa ni Janssen – subsidiary of Johnson & Johnson – Marekani.

6.  Moderna – mRNA-1273 mtengenezaji akiwa ni Moderna – Marekani.

7.  Sinopharm – SARS-CoV-2 Vaccine (Vero cell), inactivated (InCoV) Beijing mtengenezaji ni Bio-Institute of Biological Products Co Ltd – subsidiary of China National Biotec Group (CNBG)-China. 

8.  Sinovac – COVID-19 Vaccine (Vero Cell), 

Inactivated/ CoronavacTM mtengezaj ni Sinovac -China 

5. Ni chanjo zipi zimeidhinishwa na TMDA kwa matumizi nchini? 

TMDA huidhinisha chanjo ambazo zimependekezwa na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kutumika nchini. Chanjo ambazo sasa zinaruhusiwa kutumika nchini Tanzania ni pamoja na: 

 i. Janssen – Ad26.COV2.S mtengenezaji akiwa ni Janssen – subsidiary of Johnson & Johnson–Marekani. 

ii. Pfizer/BioNtech – BNT162b2/COMIRNATY Tozinameran mtengenezaji akiwa ni Pfizer/BioNtech – Marekani/Ujerumani.

iii. Moderna – mRNA-1273 mtengenezaji ni Moderna – Marekani. 

iv. Sinopharm – SARS-CoV-2 Vaccine (Vero cell), inactivated (InCoV) mtengenezaji akiwa ni Beijing Bio-Institute of Biological Products Co Ltd – subsidiary of China National Biotec Group (CNBG)-China 

v. Sinovac – COVID-19 Vaccine (Vero Cell), Inactivated/ CoronavacTM mtengenezaji akiwa ni Sinovac – China. 

6. Idhini ya matumizi ya dharura (EUL) inamaanisha nini?  

Idhini ya matumizi ya dharura (EUL) ni utaratibu uliowekwa na WHO wa kutathmini kama bidhaa mpya za afya zinafaa kwa matumizi wakati wa dharura. 

Lengo ni kufanya dawa, chanjo na vitendanishi vipatikane kwa haraka iwezekanavyo ili kushughulikia dharura iliyojitokeza bila kuathiri ubora, usalama na ufanisi wake.  Tathmini  hupima uzito wa tishio linalosababishwa na dharura na  faida inayoweza kupatikana kutokana na matumizi ya bidhaa hiyo dhidi ya athari zozote zinazoweza kujitokeza. 

Njia ya EUL inajumuisha tathmini ya kina ya taarifa za majaribio ya bidhaa husika hasa katika hatua ya II na III na vilevile taarifa nyingine za ziada juu ya usalama, ufanisi, ubora na vihatarishi vyovyote kwa kuzingatia mahitaji ya nchi za kipato cha chini na cha kati. Takwimu hizi hupitiwa na wataalamu wa WHO wasiofungamana na upande wowote wanaozingatia ushahidi wa sasa juu ya chanjo inayotathminiwa, mipango ya ufuatiliaji wa matumizi yake na mipango ya tafiti au uchunguzi zaidi. 

 Kama sehemu ya mchakato wa EUL, kampuni inayozalisha chanjo husika ni lazima ikubali kuendelea kutoa  taarifa  zaidi kuwezesha kupitishwa na WHO.  Mchakato  wa  uthibitishaji wa WHO unatathmini pia taarifa za ziada  zitokanazo na majaribio ya chanjo na msingi wake ili  kuhakikisha chanjo husika inakidhi viwango muhimu  vya ubora, usalama na ufanisi kwa watumiaji. 

7. Kuna faida gani za kupata chanjo? 

Chanjo za Covid-19 hutengeneza kinga dhidi ya virusi vya  SARS-CoV-2, hivyo kulinda mwili dhidi ya maradhi yanayosababishwa na ugonjwa wa Covid -19. 

Kutumia chanjo hii kunapunguza uwezekano wa kupata ugonjwa na kusaidia kupambana na virusi na madhara yanayoweza  kusababishwa navyo. 

Kupata chanjo pia kunalinda watu walio karibu, kwa sababu ikiwa una kinga dhidi ya maambukizi kuna uwezekano mdogo wa kuambukiza  mtu  mwingine.  Ni muhimu kulinda watu walio katika hatari kubwa ya kuugua ugonjwa wa UVIKO-19, kama watoa huduma za afya, watu wazima au wazee na watu wenye magonjwa sugu. 

8. Mtu anaweza kupewa chanjo akiwa amekwisha kuambukizwa corona? 

Hata ukiwa tayari uliwahi kuambukizwa Covid -19, unapaswa kuchanjwa kama chanjo inapatikana. Ulinzi ambao mtu anapata kutokana na kuwa na Covid-19 unatofautiana kati ya mtu na mtu, pia bado haifahamiki kinga ya asili inaweza kudumu kwa muda gani. 

9. Ufanisi wa chanjo maana yake nini? 

Ufanisi maana yake ni uwezo wa chanjo kupunguza ugonjwa kwenye kundi la watu waliochanjwa ukilinganisha na kundi la wasiochanjwa. Ufanisi hupimwa kwa kutumia majaribio yaliyofanywa kisayansi na kusimamiwa kwa  karibu. Ufanisi ni tofauti na uwezo wa chanjo kuzuia magonjwa baada ya majaribio kukamilika kwa kuwa katika kipindi hiki chanjo huonyesha inavyofanya kazi inapotumiwa na idadi kubwa zaidi ya watu. Ufanisi hupimwa tu wakati chanjo inafanya kazi katika hali fulani  ambayo pia hudhibitiwa sana. Ufanisi hutumika pia  kupima mashambulizi ya magonjwa, watu waliolazwa, idadi ya wanaoumwa na gharama za afya.  

10. Chanjo za Covid-19 zimeharakishwa na kuanza kutumika, je, kuna hatua zilizorukwa wakati wa kutengeneza chanjo hizi?  

Hakukuwa na njia fupi wala kuharakisha matumizi ya chanjo hizi. Tafiti za kisayansi kwa wanyama na binadamu zimefanyika ili kuthibitisha usalama na ufanisi wake. Kwa ujumla angalau awamu tatu za tafiti zinapaswa kufanyika kwa watu weusi na matokeo yanapaswa kuonyesha usalama na ufanisi kabla chanjo haijaruhusiwa kutumika nchini Tanzania. Taarifa zilizowasilishwa na watengenezaji zimethibitisha kwamba tafiti hizo zilifanyika.  Vilevile,  TMDA ilishiriki katika tathmini ya pamoja ya chanjo hizi  kupitia Muungano wa Mamlaka za Udhibiti wa Chanjo –  Afrika (AVAREF) ulioandaa vikao kazi vya tathmini ya chanjo husika chini ya uratibu wa WHO. 

11. Kuna haja ya kuchoma dozi zaidi ya moja na kwa nini? 

Kwa mujibu wa matokeo ya tafiti yaliyopatikana hadi sasa, chanjo ya Janssen pekee ndio  hutolewa kwa dozi moja  wakati nyingine zinahitaji dozi mbili zinazotakiwa kutumika kati  ya siku 21 au 28 kutegemeana na aina ya  chanjo. Watafiti bado wanachunguza kama kinga inapungua baada ya kuchoma dozi zilizothibitishwa hadi sasa na kama kuna haja ya kuongeza  tena.  Mara tu tafiti  zitakapokamilika, taarifa itatolewa kuhusu dozi ngapi zinatosha.  

12. Mtu anaweza kupata tena corona baada ya kuchanjwa?  

Mtu anaweza kupata tena corona baada ya kuchanjwa. Hii ni kwa sababu chanjo hizi hazina kinga ya asilimia 100 na bado utafiti unaendelea juu ya uwezo wa kuleta kinga ya muda mrefu na kupunguza maambukizi. Ndiyo maana tunapaswa kuendelea kujikinga na maambukizi sisi wenyewe na walio karibu yetu.  

13. Kuna taarifa zimesambaa kwamba chanjo hizi  zimewekewa sumaku na vifaa vya kuzuia mtu kupata mimba, je, taarifa hizi ni za kweli?  

Taarifa  hizi  si  za  kweli  na ni uzushi  unaoenezwa  pasipokuwa  na  ushahidi wowote. Haiwezekani chanjo zikawekewa sumaku au kifaa chochote cha kuzuia mtu kupata mimba. Chanjo ni kemikali za majimaji zinazoonekana kwa macho na haiwezekani kufanya hivyo. Taarifa hizo zinapaswa kupuuzwa na kuzuiwa zisienee ili kuwezesha chanjo ziweze kutumika kwa walio wengi, hivyo kuleta kinga ya ugonjwa wa corona.  

14. Inawezekana mtu aliyepata chanjo kuweza kuambukizwa kwa mara nyingine? 

Pamoja na kwamba chanjo za Covid-19 zimethibitika kuwa na usalama na ufanisi wa kuweza kuzuia watu kuugua sana na kulazwa hospitalini, bado hazijafikia asilimia 100 ya kinga.  Hivyo basi, bado kuna asilimia ndogo ya watu  waliopewa chanjo lakini wanaweza kupata corona. 

Hii inasababishwa na mambo mbalimbali kama vile tabia ya chanjo yenyewe, umri wa mtu, hali ya kiafya, kama aliwahi kuugua Covid-19, maambukizi mapya au aina ya virusi  vilivyoko nchini. Bado haijulikani kinga ya muda  mrefu ya chanjo tofauti za Covid-19 itadumu kwa muda gani? 

Kwa mantiki hii, hata kama chanjo za Covid-19 zinatolewa, lazima tuendelee kutumia mbinu zote za kiafya zinazofanya kazi kupunguza hatari ya maambukizi, kama vile kuzingatia umbali kati ya mtu na mtu, kuvaa barakoa na kunawa mikono na maji tiririka. 

Kwa siku 14 za kwanza baada ya kupata chanjo, kinga  ndiyo  inaanza  kuongezeka taratibu.  Kwa  chanjo ya  dozi  moja,  ulinzi  kwa  kawaida  hutokea  wiki  mbili  baada  ya chanjo. Kwa chanjo za dozi mbili, dozi zote zinahitajika kufikia kiwango cha juu cha kinga inayokusudiwa. 

Pamoja na kwamba chanjo hizi zimeonyesha ufanisi, bado TMDA inajifunza juu ya uwezo wa chanjo kuzuia  maambukizi na kuleta kinga ya muda mrefu. 

Kusaidia kujiweka salama wewe na wengine, endelea kuzingatia kukaa umbali wa mita moja kutoka  kwa wengine, kufunika kwa kiwiko wakati wa kukohoa au kupiga chafya, kusafisha mikono mara kwa mara kwa maji tiririka, kuvaa barakoa kwenye mikusanyiko ya watu wengi na kukaa eneo lenye mzunguko mzuri wa hewa, pia hakikisha unasoma miongozo inayotolewa mara kwa mara na  Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. 

15. Ninaweza  kutumia  chanjo  tofauti  kutoka  kwa  wazalishaji tofauti kwa wakati mmoja? 

Bado hakuna taarifa za kutosha kupendekeza mchanganyiko huu. Tafiti zinaendelea kufanyika kuangalia  kama mtu anaweza kuchomwa  dozi ya chanjo moja, kisha kuchomwa dozi ya chanjo nyingine.  

16. Chanjo hizi  zinaweza kuwalinda watu dhidi ya aina  zote za virusi vya corona?  

Utafiti zaidi unahitajika kufanyika ili kutathmini ufanisi wa chanjo za sasa za corona dhidi ya mabadiliko ya virusi. Kwa taarifa zilizopo, inaonekana chanjo nyingi huleta kinga ya kutosha dhidi ya aina za virusi vilivyoko, hasa katika kupunguza makali ya ugonjwa, kulazwa hospitalini na vifo.  

Tafiti  bado  zinaendelea  kuangalia  aina  ya  virusi  na namna  vinavyojibadilisha  ili kufanya mabadiliko ya chanjo kuweza kuendelea kuleta kinga kwa watu wengi. Kwa hali ilivyo sasa, idadi kubwa ya aina za virusi vilivyoko vinaweza kuzuiwa na chanjo zilizoko kusababisha ugonjwa mkali.  

17. Baada ya kuchanjwa tunapaswa kuendelea kujitenga, kusafisha mikono na kuvaa barakoa tena, kwa nini? 

Chanjo zimekuja kusaidia katika mapambano dhidi ya corona. Pamoja na kwamba chanjo hizi zipo kwa  sasa,  tunapaswa  kuendelea  kuvaa  barakoa,  kunawa  mikono mara kwa mara kwa maji tiririka, kukaa eneo lenye hewa nzuri, kuzingatia umbali na kujiepusha na mikusanyiko. 

18. Kinga ni ya muda gani baada ya kuchanjwa?

Si chanjo zitakazodhibiti ugonjwa  bali  uchanjaji.  Wizara  kupitia  IVD  inafanya  kazi kuhakikisha  upatikanaji  wa  chanjo  kwa  haki  na  usawa,  na  kuhakikisha  kila  mtu anapata  kinga kwa  kuanzia na  walio  hatarini zaidi.  Hata hivyo, ikumbukwe kuwa kupata chanjo si lazima, ni hiari kwa watu ambao wako tayari kuchanjwa. 

Kwa sababu chanjo za corona zimetengenezwa hivi karibuni tu, ni mapema kujua muda wake wa kinga. Utafiti unaendelea kujibu swali hili. Hata hivyo, inatia moyo  kwamba taarifa zinazopatikana zinaonyesha kuwa watu wengi wanaopona corona hutengeneza kinga ambayo hutoa angalau kipindi fulani cha ulinzi dhidi ya kuambukizwa tena, ingawa wanasayansi bado wanajifunza  jinsi  ulinzi  huu ulivyo, nguvu yake na inachukua muda gani. 

19. Chanjo za corona ni salama kwa matumizi ya binadamu? 

Kama chanjo yoyote ilivyo, chanjo za corona zinaweza kusababisha athari chache, za  muda mfupi, kama  vile  homa  ya  kiwango cha chini,  maumivu  au  ngozi  kuwa nyekundu eneo ulipochomwa sindano. Athari hizi ni za kawaida na huisha baada ya siku chache. Madhara  makubwa  au  ya  kudumu ya chanjo yanawezekana  lakini  ni nadra sana kutokea. TMDA inaendelea kufuatilia usalama wa chanjo hizi ili kuangalia madhara yanayoweza kujitokeza baada ya matumizi  ya  muda mrefu kwa  lengo  la kulinda afya ya jamii.  

Madhara  yaliyoripotiwa  hadi  sasa  ni  ya  wastani na yanajumuisha homa, uchovu, maumivu ya kichwa, maumivu ya misuli, baridi, kuhara na maumivu kwenye sehemu palipochomwa sindano. Madhara haya yanatofautiana na aina ya chanjo.  

Madhara haya yanatibika kwa kupumzika, kunywa maji mengi na kutumia dawa zenye paracetamol au acetaminophen. Ikiwa madhara yatazidi saa 24, watumiaji wawaone wataalamu wa afya kwa uchunguzi zaidi. 

 Endapo mtu atapata shida ya kupumua,  maumivu ya kifua, kuchanganyikiwa,  kushindwa kuongea au  kushindwa kutembea, ni vema kuwahi kituo cha afya kilicho karibu kwa msaada zaidi.  

20. Chanjo za mRNA ni salama? Ikiwa zinatengenezwa kwa teknolojia mpya, tunawezaje kuwa na uhakika? 

Chanjo za corona za mRNA zimechunguzwa kwa teknolojia ya hali  ya  juu  na kuthibitika kuwa na ufanisi wa kuzuia ugonjwa wa Covid-19. 

Teknolojia ya kutengeneza chanjo za mRNA imetumika miaka mingi na imehusisha pia uvumbuzi wa chanjo nyingine kama za ugonjwa wa zika, kichaa cha mbwa na mafua. Chanjo za 

mRNA hazina virusi vya corona na haziingiliani na DNA ya binadamu. 

21. TMDA itafuatiliaje usalama wa chanjo hizi?  

TMDA ina  mifumo miwili  ya  ufuatiliaji wa bidhaa kwa ajili  ya  kuhakikisha usalama wake. Hii ni pamoja na ufuatiliaji wa hiari na ule wa karibu. 

Mfumo wa ufuatiliaji usalama wa hiari hutumia fomu za njano (kwa watoa huduma za afya) na fomu za kijani (kwa wagonjwa) kuripoti madhara ya dawa na chanjo (ADRs). 

Njia ya ufuatiliaji wa karibu (CEM) hutumia fomu maalumu zilizoandaliwa kutegemeana na aina ya ugonjwa na dawa inayotumika. Njia ya CEM hutumiwa kwa dawa na chanjo mpya zilizoingizwa ikiwa ni pamoja na zile zinazotumiwa na watu wengi. 

TMDA itatumia njia ya CEM kufuatilia usalama wa chanjo za UVIKO-19 ili kurekodi matukio yote pamoja na madhara ya muda mrefu ya chanjo.  

 Pamoja  na  hayo,  mfumo wa kuripoti  madhara kwa hiari  pia utatumika ili  kutambua madhara mengine yote yanayoweza  kujitokeza wakati  chanjo  hizi zinatumika hapa nchini. Ufuatiliaji utafanywa kwa kushirikiana na Mpango wa Chanjo wa Taifa (IVD) ambao uko chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. 

22. Mtu anapaswa kuripoti madhara ya kiafya yanayotokea baada ya chanjo na nini kitatokea ikiwa tukio baya litaripotiwa? 

 Kama ilivyo kwa chanjo nyingine, TMDA inafuatilia kwa karibu usalama na ufanisi wa chanjo zote zinazotumika katika programu za chanjo. Ikiwa shida ya kiafya itaripotiwa kufuatia matumizi ya chanjo, uchunguzi wa kina hufanywa na TMDA kwa kushirikiana na  IVD. Fomu  za CEM  za kukusanya  taarifa  za usalama wa chanjo za Covid – 19 zitatumika (zinapatikana www.tmda.go.tz). 

Hata  hivyo,  ni  nadra  kukuta shida za kiafya  zinazotokea baada  ya  kuchanjwa kuthibitika kuwa kweli husababishwa  na  chanjo  yenyewe.  Shida za kiafya kufuatia chanjo mara nyingi hutokea kwa bahati mbaya na mara nyingi hazihusiani moja kwa moja na chanjo.  

Wakati  mwingine zinahusiana  na  jinsi  ambavyo chanjo husika imehifadhiwa,  kusafirishwa au kusambazwa.  

Makosa  yanayohusiana  na  utoaji  wa chanjo yanapaswa kuzuiwa kwa kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya pamoja na kuimarisha mnyororo wa usambazaji. Hata hivyo, endapo madhara ya chanjo yatatokea, TMDA itachukua hatua kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu. Uchunguzi zaidi utafanyika pia ili kubaini ni nini hasa kilichosababisha madhara hayo na hatua za kurekebisha zitawekwa. 

23. Kuna tahadhari zozote za kuchukua kabla ya kutumia chanjo hizi? 

Chanjo za corona ziko salama kwa watu wengi wenye umri wa miaka 18 na zaidi, ikiwa ni pamoja na wenye magonjwa mengine kama vile shinikizo la damu, kisukari, pumu, mapafu, homa ya ini na ugonjwa wa figo. 

Pamoja na hilo, mtumiaji atapaswa kuchukua tahadhari ikiwa ana upungufu wa kinga mwilini, mtu ana ujauzito au kunyonyesha, ana historia ya mzio, hasa kwa chanjo husika au viambata vyake au ana udhoofu wa mwili. 

24. Tunaweza kuacha kuchukua tahadhari baada ya chanjo? 

 Chanjo  inatoa  kinga dhidi ya kupata maambukizi  makali  na kifo.  Kwa  siku  14  za mwanzo baada ya kupata chanjo, mtu hatakuwa na kiwango kikubwa cha ulinzi, kwa kuwa huongezeka taratibu. Kwa chanjo za dozi moja, kinga kwa kawaida itatokea wiki mbili  baada ya chanjo.  Kwa chanjo za dozi mbili,  dozi zote zitahitajika  ili  kufikia kiwango cha juu cha kinga inayotakiwa. 

Wakati chanjo ya corona itakukinga na maambukizi makali na kifo, bado tunajifunza juu  ya  kiwango  gani  kitakuzuia kuambukizwa  na  kusambaza virusi  kwa wengine. Takwimu kutoka nchi nyingine zinaonyesha kuwa chanjo zinazotumika sasa zinalinda dhidi ya hali ya ugonjwa mkali na kulazwa hospitalini.  Hata hivyo, hakuna chanjo yenye ufanisi wa asilimia 100. 

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na TMDA bado  tunaendelea kufuatilia mabadiliko ya  aina ya virusi vilivyopo nchini na uwezo wa muda mrefu wa chanjo zilizovumbuliwa. Kwa sababu hizi, na kwa kuwa wengi katika jamii bado hawataweza kupata chanjo, kuendeleza hatua nyingine za kuzuia ni muhimu hasa katika jamii ambazo mzunguko wa virusi ni mkubwa. 

Ili kukusaidia wewe na wengine kuwa salama, na wakati juhudi zinaendelea kupunguza maambukizi ya virusi na kuongeza chanjo,  unapaswa kuendelea kuzingatia kukaa umbali  wa mita 1 kutoka kwa wengine,  kukohoa au kupiga chafya kwenye kiwiko chako, kusafisha mikono yako mara kwa mara, kuvaa barakoa, kuepuka misongamano na kukaa maeneo yenye mzunguko mzuri wa hewa. Wakati wote fuata miongozo inayotolewa na  Wizara na  IVD  kulingana  na  hali na hatari ya mahali unapoishi. 

25. Chanjo ya corona inatolewa kwa watoto wa umri gani?  

Chanjo ya corona haitolewi kwa watoto bali kwa wenye umri unaoanzia miaka 16. Umri huu ndio imethibitika kuna maambukizi mengi ya ugonjwa wa Covid-19 na tafiti za usalama na ufanisi wake zimefanyika kuanzia kundi hili hadi miaka zaidi ya 60.  

26. Mtu akiwa na Covid -19 anaweza kuchangia damu?  

Mtu mwenye UVIKO-19  anayetaka  kuchangia damu  ni vema kupata ushauri  wa kitaalamu kabla ya kufanya hivyo.  

27. Watu wa vijijini watapataje chanjo?  

Chanjo ya UVIKO-19 imeanza kutolewa kwenye vituo ambavyo vimeainishwa kupitia IVD iliyoko chini ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Ni vema kufika vituo vya kutolea huduma za afya ili kufahamu mahali chanjo inapotolewa.  

28. Chanjo ni njia inayotumiwa na mataifa makubwa kupunguza idadi ya watu na ilitengenezwa kwa ajili ya kupunguza watu duniani?  

Chanjo ya Covid -19 imetengenezwa kwa lengo la kuleta kinga dhidi ya corona, si kuangamiza watu.  Kuna chanjo  nyingi  pia zilizotengenezwa  na mataifa hayo hayo makubwa na hadi leo haziui watu bali zinakinga watu dhidi ya magonjwa mbalimbali kama vile surua, tetekuwanga, polio, tetenasi, kichaa cha mbwa, saratani ya shingo ya kizazi, homa ya ini na kadharika.  Huu  ni  uvumi  tunaopaswa  kuuacha  ili tuweze kuwalinda Watanzania wasipate maambukizi ya ugonjwa mkali wa Covid-19.  

29. Kama unatarajia kupata ujauzito bado unaweza kupata chanjo? 

 Kwa tafiti ambazo zimefanyika hadi sasa, chanjo ya Covid-19 haijaonekana kuleta madhara  kwa mjamzito wala mtu anayetarajia kubeba ujauzito. Hata hivyo  tafiti zinaendelea kufanyika kuona kama zinaleta  madhara  kwa wajawazito baada  ya matumizi ya muda mrefu.  

30. Nani anadhibiti chanjo Tanzania?  

Sheria ya Dawa na Vifaa Tiba, Sura 219 imeipa mamlaka TMDA kudhibiti chanjo za binadamu na mifugo pamoja na chanjo za Covid-19. Udhibiti unahusisha usajili wa chanjo,  udhibiti  wa  uingizaji nchini  na  usafirishaji nje ya nchi,  ufuatiliaji ubora  na usalama katika soko, ukaguzi, utoaji leseni za majengo yanayojihusisha na masuala ya chanjo, uchunguzi wa kimaabara na udhibiti wa majaribio ya chanjo. 

By Jamhuri