Ugomvi umeibuka baina ya watayarishaji wa Mbio za Soweto Marathon nchini Afrika Kusini, wakisema hazitafanyika Novemba 3, mwaka huu.

Wakati hayo yakiendelea, Rais wa Shirikisho la Riadha Afrika Kusini, James Evans, amesema mbio hizo zitaendelea kama ilivyopangwa. Vijana wa Soweto Marathon Trust walioanzisha mbio hizo, wamesema kuna wasiwasi kuwa Evans huenda akazipeleka mbio hizo mjini Cape Town anakotokea, lakini kamwe hazitafanyika Soweto.

 

Wanamlaumu Evans kwa kutumia pesa za kuandaa mbio hizo kwa mambo mengine, na pia anaonekana kama hataki kusema kiasi kilichotolewa na wafadhili.

 

Hata hivyo, Evans anasema baadhi ya ripoti zinazosema kuwa mbio hizo zimefutiliwa mbali na Soweto Marathon Trust, ni sehemu ya njama ya kutaka kumng’oa madarakani.

 

Mfuko wa Soweto Marathon Trust unahitaji dola 500,000 kuandaa mashindano hayo yaliyoanzishwa mwaka 1991 yakiwa maarufu kupita yote barani Afrika. Mshindi wa mbio hizo mwaka jana alikuwa Shadrack Kemboi wa nchini Kenya.

 

Sasa Soweto Marathon Trust wanamtaka Waziri wa Michezo wa Afrika Kusini, Fikile Mbalula (Vuvuzela), aingilie kati katika kuhakikisha kuwa hali inakuwa shwari.

By Jamhuri