📌Mhe. Salome awapongeza waandaaji wa shindano kwa kuibeba ajenda ya nishati safi ya kupikia kitaifa na kimataifa.

Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, amewapongeza washiriki wa shindano la urembo la Miss Universe Tanzania kwa jitihada zao za kuwa mabalozi wa Nishati Safi ya Kupikia kwa kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kutumia nishati hiyo nchini.

Mhe. Salome amesema Serikali itaendelea kushirikiana na jukwaa hilo muhimu katika kuifikisha ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia kwa wananchi, huku akiwataka washiriki 33 wa shindano hilo kuwa chachu ya kufikisha ujumbe sahihi kwa jamii, hususan katika maeneo ya vijijini.

Ametoa kauli hiyo Agosti 23, 2026 jijini Dar es Salaam wakati wa shindano la Miss Universe Tanzania lililofanyika katika Hoteli ya Ledger Plaza kwa lengo la kupata warembo 20 watakaoendelea na hatua inayofuata ya mashindano hayo, kuelekea kumpata mwakilishi wa Tanzania katika shindano la Miss Universe duniani.

Amesema ushiriki wa warembo hao katika kampeni ya Nishati Safi ya Kupikia unatoa fursa muhimu ya kuifikisha ajenda hiyo kwa makundi mbalimbali ya jamii na kuongeza uelewa kuhusu faida za kutumia nishati salama, nafuu na rafiki kwa mazingira.

Mhe. Salome ameeleza kuwa Ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia, inayopewa msukumo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, inalenga kuhakikisha angalau asilimia 80 ya Watanzania wanatumia nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2034.

Ameongeza kuwa matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini yameongezeka kutoka takribani asilimia 6 miaka michache iliyopita hadi asilimia 28.6 kwa sasa.

Aidha, Mhe. Salome amempongeza Mkurugenzi wa Taifa wa Miss Universe Tanzania, Bi. Millen Magese, kwa kuunganisha mashindano hayo na ajenda ya Nishati Safi ya Kupikia, pamoja na kuwashukuru wadhamini wanaounga mkono jitihada hizo.

Pia ametoa wito kwa kampuni na wadau wengine kujitokeza kuunga mkono mashindano hayo ili yaweze kuwafikia wanawake wengi zaidi na kupanua wigo wa uhamasishaji.

Kwa upande wake, Bi. Magese amesema Miss Universe Tanzania imeamua kubeba ujumbe wa Nishati Safi ya Kupikia mwaka 2026 ikiwa ni sehemu ya ushirikiano na Serikali katika kuongeza uelewa na kuhamasisha matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.

Amesisitiza kuwa Miss Universe Tanzania itaendelea kushirikiana na Serikali pamoja na wadau wa maendeleo kuhakikisha ujumbe wa Nishati Safi ya Kupikia unaendelea kuwa sehemu ya mashindano hayo kila mwaka, hivyo kuwapa washiriki nafasi ya kuwa mabalozi wa mabadiliko katika jamii.

Katika shindano hilo, washiriki walipata nafasi ya kutoa jumbe mbalimbali kuhusu Nishati Safi ya Kupikia, wakieleza umuhimu wa Watanzania kuhamia katika matumizi ya nishati salama, nafuu na rafiki kwa mazingira.

Wamesisitiza kuwa wataendelea kutumia nafasi zao kama mabalozi kuelimisha na kuhamasisha jamii ili kuchangia kupunguza matumizi ya nishati isiyo safi ya kupikia na kufanikisha malengo ya kitaifa.