MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA AIKOMALIA CHADEMA, AITAKA KUJIELEZA KWANINI ASIKICHULIE HATUA

Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi kwa mara nyingine ametoa siku tano kwa Chadema kujieleza kwa nini asikichukulie hatua kwa kukiuka sheria na kanuni za maadili ya vyama vya siasa.

Katika barua hiyo ya Jaji Mutungi ya Machi mosi, 2018 iliyopokelewa Chadema Machi 2 inatakita chama hicho kikuu cha upinzani nchini, kujieleza kwa nini kilivunja sheria na kanuni hizo Februari 16, 2018.

Barua hiyo ya Jaji Mutungi inatokana na kutoridhishwa na majibu ya barua yake ya Februari 21 aliyokiandikia chama hicho, akikipa siku tano kujieleza kwa nini kilivunja sheria na kanuni hizo.

Akizungumza na Mwananchi Digital leo Machi 4, 2018, mkurugenzi wa itifaki, mawasiliano na mambo ya nje wa Chadema, John Mrema amesema barua hiyo wameipokea jana na kesho wanatarajia kuijibu.