Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dar es Salaam
Bohari ya Dawa (MSD) inatarajia kuokoa zaidi ya Sh bilioni 2.3 kwa mwaka, ikiwa ni gharama ambazo zimekuwa zikitumika kukodisha maghala binafsi kwa ajili ya kuhifadhia bidhaa za afya.
Tathimini hiyo imetolewa na uongozi wa MSD baada ya kukabidhi rasmi hati ya mradi wa ujenzi wa ghala jipya la kisasa (site), pamoja na kibali cha ujenzi kwa Kampuni ya Hainan International kutoka China, cha ujenzi wa ghala jipya na la kisasa la Kanda ya Dar es Salaam.
Ujenzi wa ghala hilo la kisasa lenye ukubwa wa mita za mraba 3,900, unatekelezwa katika eneo la Keko, karibu na Makao Makuu ya MSD mkoani Dar es Salaam, na unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi 12 kutoka sasa.
Akizungumzia ujenzi huo, Mkurugenzi Mkuu wa MSD Mavere Tukai alisema mradi huo umezingatia matumizi ya teknolojia za kisasa na nishati mbadala ili kuongeza ufanisi wa matumizi ya nishati, kupunguza gharama za uendeshaji na kuunga mkono jitihada za uhifadhi wa mazingira.
Aliongeza kwamba fedha zote za utekelezaji wa mradi huo zipo tayari, jambo linalotoa uhakika wa mradi kukamilika kwa wakati.
Kukamilika kwa ghala hilo kutaimarisha uwezo wa MSD wa kuhifadhi na kusambaza bidhaa za afya, kuongeza ufanisi wa huduma kwa wateja na wadau wa sekta ya afya, pamoja na kuimarisha upatikanaji wa bidhaa za afya kwa wananchi.









