Mtibwa Sugar Wawapania Azam, Kombe la FA

Kocha Mkuu wa Mtibwa Sugar, Zuberi Katwila amejipambanua na amesema wamejiandaa vizuri kuhakikisha leo lazima wawafunge Azam FC na kutinga hatua ya Nusu Fainali Kombe la FA.

Mtibwa Sugar inacheza mechi ya robo fainali ya Kombe la FA kwenye Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam na Katwila anaamini wamejiandaa hasa.

“Azam wana timu nzuri lakini kweli tumejiandaa sana na tuko Dar es Salaam kutafuta matokeo ya mechi hiyo,” alisema.

Mchezo huo unatarajiwa kuwa na ushindani mkubwa kutokana na uwezo wa wachezaji wa timu hizo ambao wamekuwa wakiuonyesha katika mchuano hiyo na Ligi Kuu Bara msimu huu.

Mshindi katika mechi hiyo ataingia nusu fainali ya michuano hiyo ambayo bingwa wake atapata nafasi ya kuiwakilisha Tanzania katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika mwakani.