Mtoto wa Kova yumo

Kielelzo1Sakata la wizi na upotevu wa makontena limechukua sura mpya baada ya vituko kadhaa kujitokeza ikiwamo watuhumiwa ambao ni watoto wa vigogo kupata dhamana kimizengwe.

Ukiacha hilo, watendaji walioteuliwa na aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Badari, Madeni Kipande kusimamia upakiaji na upakuaji wa makontenda kisha yakaanza kupotea kwa kiwango cha kutisha na mengine kuibwa, mpango umesukwa na sasa ndiyo wanaokaimu nafasi nyeti bandarini.

Mwanzo, Waziri Mkuu Majaliwa Kassim alibaini upotevu wa makontena 329 yaliyoitia Serikali hasara ya wastani wa Sh bilioni 12, baadaye wakagudua makontena 2,387. Ilipofikia hatua hii, Mkurugenzi Mkuu wa Bandari, Awadhi Massawe akaagiza ufanyike uchunguzi wa kina, na uchunguzi aliobaini upotevu wa makontena 11,884 yaliyolitia taifa hasara ya Sh bilioni 47.4 na magari 2,019 yalitolewa bila kulipiwa kodi au ushuru. Makontena haya 11,884 yamebainishwa na Profesa Makame Mbarawa, Waziri mwenye dhamana ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano baada ya uchunguzi alioagiza Massawe.

Kutokana na hali hiyo, Watumishi 7 wa bandarini iliamuriwa wakamatwe na Jeshi la Polisi na wengine 8 wakatoroka na wanaendelea kutafutwa na Jeshi la Polisi. Kati ya hao saba waliokamatwa yumo mtoto wa aliyekuwa Kamanda Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, anayeitwa kwa jina la Masoud Suleiman Kova.

JAMHURI limepata malalamiko kutoka kwa wafanyakazi wa Bandari na watu walioko ndani ya Jeshi la Polisi wakihoji ilikuwaje mtoto wa Kova, aliyehusishwa na upotevu wa makontena amekamatwa na kupewa dhamana usiku wa Desemba 29, 2015 huku baadhi ya wakurugenzi waliokamatwa awali wakilazwa ndani.

Masoud alikamatwa pamoja na John Elisante, Leticia Masaro, Christina Temu, Merina Chawala, Adnan Ally na Benadeta Sangwe.

Watuhumiwa wengine wanane waliodaiwa kukimbia na wanaendelea kutafutwa walitajwa kuwa ni Happygod Naftal, Nathan Edward, Aron Lusingu, Amani Kazumari, John Mushi, Valentine Sangwe, Bonasweet Kimaima na Zainab Bwijo.

“Watu wanauliza mbona kuna watu wanatolewa kafara? Kuna mtoto huyu wa Kova, Masoud Suleiman Kova. Yeye ni jipu kubwa tu, na yeye ndiyo pilot kwenye mambo haya kule kwenye ICDs. Sasa jana walikamatwa, lakini kundi lake hawakuwekwa ndani, unaona ehee?

“Yaani wameripoti tena asubuhi leo wakaenda kukaguliwa. Wakati kuna senior most officials (maafisa waandamizi) wa TPA waliwekwa ndani. Labda kwa sababu huyu ni mtoto wa Kova, hili inabidi nalo bwana tulipigie sauti. Kusiwe na double standards,” anasema mmoja wa wafanyakazi wa TPA.

Mfanyakazi mwingine wa TPA anasema: “Huyu mtoto wake [Kova] alilala nyumbani. Wakati akina Mdoe, akina nani wakurugenzi wote wa TPA walilala ndani… wamekwenda kumkagua wakarudisha taarifa kuwa hawakukuta kitu chochote nyumbani kwake hata kijiko? Hata gari alilonunua Sh milioni 60 RAV4? This should be a jockey (huu ni utani),” alisema mtoa habari wetu.

Inaelezwa kuwa baadhi ya askari walipinga utaratibu uliotumika kumkagua mtoto wa Kova, kwani kwa kumruhusu kwenda kulala nyumbani yeye na wenzake walipata fursa ya kwenda nyumbani kuhamisha kila kilichokuwapo. “Wenzake wanasema wakifikishwa mahakamani watasema kila kitu na hiyo RAV4 aeleze alipata wapi fedha,” anasema. Msoud amepewa dhamana na anaripoti polisi na wenzake kila baada ya siku mbili wakati uchunguzi unaendelea.

 

Kova atoa kauli

Juhudi za kumpata Masoud hazikuzaa matunda, ila JAMHURI lilimtafuta Kova kuhusiana na ukiukwaki wa taratibu za ukamataji, kuhoji na kupekua kuhusiana na mtoto wake, Kova alisema: “Kwanza nikukatishe kauli…

“Watuhumiwa wote ninavyozungumza na wewe wako nje. Kuwe kuna ndugu wa Kova, au hakuna ndugu wa Kova wote wako nje, kwa hiyo usitaje mtuhumiwa mmoja mmoja. Halafu suala la pili, ni kuhusu maadili. Hivi ni kweli maadili ya vyombo vya habari yanaweza kwenda sawa hapo kwa kesi ya mtu mwingine kumpa mwingine?

“Ninachokifahamu mimi ni kwamba JAMHURI ni gazeti kubwa, gazeti hili sasa limejijengea heshima, sidhani kama linafuata mijadala ya kwenye mitandao na kuanza kuandika habari.

“Nyie Waandishi na Wahariri wa Habari ni watu wanaofuata maadili. Hata juzi nimezungumza na (jina la mhariri linahifadhiwa – si wa JAMHURI) … akasema kabisa kwamba this is unethical (kinyume cha maadili) kumtaja Kova kwa kesi ya mtu mwingine [mtoto wake].

“Suala la kumtaja mtu mwingine linaweza kufananishwa na sakata la uhuru Kenyatta. Kuna watu walianza kumsakama eti baba yake alifanya hivi au vile, lakini leo Uhuru ni Rais Kenya. Kisheria huwezi kumkamata mtu mwingine kwenye kesi ya mtu mwingine,” anasema.

JAMHURI lilimhoji Kova juu ya taarifa kuwa mtu au chombo chochote kinachofuatilia mambo yake au ya ndugu na jamaa zake anao utaratibu wa kuadhibu wahusika kwa kuwapoteza duniani, naye akasema:

“Aaah, hakuna kitu kama hicho, lakini sheria inampa mtu nafasi ya kujitetea akiona anaonewa, sasa kama naonewa, nikae kimya?”

Novemba, mwaka jana Waziri Mkuu Kassim Majaliwa alibainisha kuwa ukaguzi uliofanywa Julai 30, mwaka huu uligundua kuwapo kwa mianya mingi ya ukwepaji kodi yakiwamo makontena 2,387 yaliyopitishwa kati ya Machi na Septemba mwaka jana kinyume cha taratibu.

Majaliwa akifanya ziara ya kushitukiza bandarini Dar es Salaam Novemba 27, mwaka jana. Alifichua mwanya wa ukwepaji kodi kwa makontena 329 yenye thamani ya wastani wa Sh bilioni 12. Aliwasimamisha kazi baadhi ya maofisa wa TRA; na muda mfupi baadaye Rais John Magufuli, akamsimamisha kazi Kamishna Mkuu wa TRA, Rished Bade.

Kwa upande wa TPA aliowasimamisha kutoka idara ya usimamizi wa ICD ni Happygod Naftari, Juma Zaar, Mkango Alli na Steven Mtui. Wengine ni Titi Ligalwike, Lyidia Kimaro, John Elisante na James Kimwomwa.

Kwa upande wa viongozi waliotoa ruhusa kwa makontena hayo kuondoshwa bandarini nao wamesimamishwa. Hao ni aliyekuwa Meneja Mapato ambaye alikuwa amehamishiwa Kitengo cha Fedha cha Makao Makuu, Shaaban Mngazija, aliyekuwa Mkurugenzi wa Fedha na Mkuu wa Bandarikavu ambaye pia alikuwa amehamishiwa Makao Makao Makuu kuwa Naibu Mkurugenzi Huduma za Biashara, Rajab Mdoe.

Wengine ni Kaimu Mkurugenzi wa Fedha, Ibin Masoud na Meneja Bandari Msaidizi Fedha, Apolonia Mosha.

Rais John Magufuli alitengua uteuzi wa Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Dk. Shaaban Mwinjaka kwa kushindwa kusimamia TPA na Kampuni ya Reli Tanzania (TRL).

Pamoja na Mwinjaka, Rais Magufuli pia alitengua uteuzi wa Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Awadhi Massawe. Pia alivunja Bodi ya Wakurugenzi ya TPA na kutengua uteuzi wa Mwenyekiti wa Bodi ya TPA Profesa Joseph Msambichaka.

Wajumbe wa Bodi waliotenguliwa walikuwa ni Naibu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson, aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa EWURA, Haruna Masebu, Dk. Francis Michael, Mhandisi Gema Modu, Mhandisi Musa Ally, Nyamsingwa, Crescentius Magori, Flavian Kinunda na Donata Mugassa.

 

Watoa taarifa walimkomoa Massawe

Uchunguzi unaonyesha kuwa aliyepeleka taarifa za upotevu wa makontena kwa Waziri Mkuu Majaliwa alipiga hesabu za mbali akilenga kumkomoa Mkurugenzi Mkuu wa Bandari, Awadhi Massawe aliyekuwa ameshika wadhifa huo ndani ya miezi miwili tangu kuthibitishwa kwake.

Massawe alianzisha safisha safisha Bandari baada ya kupata wadhifa huo kwa kufanya mabadiliko makubwa ikiwamo kuwashusha vyeo ‘waliomchoma’, kurejesha nidhamu bandarini, kuhamisha watumishi 30 katika kitendo cha fedha na kurejesha kazini idadi kubwa ya watumishi waliokuwa wameondolewa na Madeni Kipande kwa chuki.

“Huyu mtu alipeleka taarifa hizi kwa Waziri Mkuu, akishirikiana kwa karibu na waliokuwa wasaidizi wa Kipande, na kweli wamefanikiwa maana wamepeleka nusu taarifa, Massawe amewajibishwa kwa kosa lisilo lake na wapambe wa Kipande wanaowasiliana naye kila siku na walioshiriki kupoteza makontena wameteuliwa kukaimu nyadhifa nyeti,” anasema mtoa taarifa wetu.

Kaimu Mkurugenzi wa sasa wa TPA, Eng. Aloyce Matei, aliyeteuliwa kushika wadhifa huo badala ya Massawe imeelezwa kuwa alipelekwa Bandari na Kipende kwa shinikizo la aina yake bila kufuata taratibu za ajira serikalini na akapewa nafasi ya Naibu Mkurugenzi wa Bandari (Miundombinu).

“Kipande alikuwa hawezi kufanya uamuzi wowote bila kumshirikisha huyu Matei maana alikuwa mkono wake wa kuume. Kwa vyovyote vile na kwa kuwa Naibu wake, na kwa jinsi wanavyoendelea kuwasiliana kwa ukaribu hata uki-print out mawasiliano yao, basi utaona aliyosema Kipande kuwa atarudi Bandari hata kama kupitia mgogo wa mtu mwingine, hili limefanikiwa,” anasema mtoa taarifa wetu.

Kwa siku chache, ambazo Matei amekaimu wadhifa huo, tayari inaelezwa amekwishaanza kuwatenga wakurugenzi wa idara nyingine isipokuwa idara moja tu ya fedha, anasema mtoa taaria wetu.

 

Chanzo cha makontena kupotea

Kipande wakati akiwa Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TPA alipitisha waraka uliozaa matatizo yote yanayoshuhudiwa sasa bandarini. Awali Bandari ya Dar es Salaam ilikuwa ikisimamia upakuaji na upakiaji wa makontena, lakini Kipande akahamishia majukumu hayo makao makuu.

Kipande aliyekuwa na urafiki mkubwa na Waziri wa Uchukuzi wa wakati huo, Dk. Harrison Mwakyembe, Februari 5, mwaka 2013 aliiandikia Bandari ya Dar es Salaam kuieleza rasmi kuwa ameunda Kamati Maalum hivyo jukumu la makontena limechukuliwa na makao makuu.

Katika barua hiyo yenye Kumb. Na DG/3/3/06 (nakala tunayo) Kipande alimtaka Mkurugenzi wa Utumishi ndugu P. D. Gawile kwa kushirikiana na wakurugenzi wengine kusimamia kitengo cha makontena hasa TICTS, ICDs na CFS.

Jukumu la Makontena alilikabidhi kwa barua mikononi mwa Mkuu wa Ulinzi – Swange, Mkurunzi wa Fedha – Rajah Mdoe (amesimamishwa), Mkurugenzi wa Mawasiliano na Teknohama –  Phares Magessa (ameshushwa cheo), Mkurugenzi wa Utekelezaji – Hebel Mhanga (Sasa ndiye Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam) na Mkuregenzi wa Huduma za Sheria – Kokutulage Kazaura.

Wakati huo, Massawe alikuwa Meneja wa Bandari ya Dar es Salaam na kumbukumbu zinaonyesha upotevu wa makontena ulikuwa ni wastani wa makontena 4 kwa mwaka, lakini baada ya Kipande kuunda Kamati hii ya wakurugenzi mwaka 2013, kwa mwaka 2014 upotevu wizi wa makontena umefikia karibu 14,000 kwa mwaka.

 Katika barua hiyo, Kipande alidai anaipunguzia Bandari ya Dar es Salaam mzigo, anaiepusha na mgongano wa masilahi na uamuzi wake huo ulilenga kuongeza ufuatiliaji, utendaji na mapato.

Uchunguzi wa JAMHURI umebaini kuwa mwaka 2013 baada ya uamuzi huo wa Kipande makontena 4,200 na magari 919 vilipitishwa bila kulipiwa ushuru. JAMHURI ina nyaraka za ripoti ya uchunguzi zinazothibitisha madai hayo.

Kipande, aliondolewa kwenye wadhifa huo na aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta, kutokana na tuhuma za ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka.

Wataalam wa masuala ya sheria waliozungumza na JAMHURI, wameeleza mshangao wao kwa nini hadi leo Kipande hajakamatwa. “Haiwezekani mtu aliyefanya uamuzi wa ovyo kiasi hiki, leo aendelee kuwa kazini. Wanasulubiwa watu wengine, lakini yeye anaendelea kucheka tu yuko uraiani. Hili haliwezekani,” alisema mmoja wa watu hao waliohojiwa na kutaka Kipande akamatwe haraka kwani amelitia taifa hasara kubwa.

Kinachotokea Bandari ya Dar es Salaam kinathibitisha kauli aliyopata kuitoa Rais wa Rwanda Paul Kagame kuwa iwapo angekabidhiwa Bandari hii, basi angeweza kujitosheleza bajeti ya nchi kwa kutumia Bandari moja tu ya Dar es Salaam kwa maana kwamba ufanisi wa Bandari uko chini na watu wanawaza kuiibia Bandari badala ya kukusanya mapato ya nchi.