Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Mwanza

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mwanaidi Ali Khamis amesema Serikali inaendelea kuwekeza na kutekeleza jitihada mbalimbali zinazolenga kujenga jamii yenye usawa wa kijinsia.

Mwanaidi ameyasema hayo Oktoba 29, 2023 wakati wa maadhimisho ya Jubilee ya maiaka 25 ya Shule ya Sekondari Loreto iliyopo Nyakato Mkoani Mwanza.

Amesema kuwa, Serikali inawekeza kwa kuweka uwiano wa kunufaika sawa katika fursa za elimu na uchumi kati ya wanaume na wanawake ili kuimarisha upatikanaji wa haki na kupunguza ukatili wa kijinsia katika jamii ikiwemo kutoa elimu na mafunzo ya stadi za maisha ikiwa ni hatua madhubuti ya kuiishi falsafa ya elimu na kujitegemea.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mwanaidi Ali Khamis akiwa katika picha ya pamoja na watumishi wa Shule ya Sekondari Loreto iliyopo Nyakato Mkoani Mwanza wakati wa maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25 ya Shule hiyo yaliyofanyika Oktoba 29, 2023.Picha zote na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini WMJJWM

“Pamoja na jitihada zinazofanywa na Serikali na kuungwa mkono na wadau wa maendeleo zinazolenga kumkomboa, kumlinda na kumuwezesha msichana wa kitanzania kufikia maisha yake kwa utimilifu, bado vipo vikwazo vya kijamii, kitamaduni na kiuchumi vinavyorudisha nyuma jitihada hizo” amesema Naibu Waziri Mwanaidi

Aidha amewasihi wanafunzi Shuleni hapo kuzingatia mafunzo na mahusia ya walimu na wazazi kwa mustakabali wa maendeleo binafsi na taifa kwa ujumla, kumtanguliza Mungu katika mahitaji yao na kuenzi mafundisho mema mnayopatiwa ndani na nje ya eneo la shule.

Naye Mkuu wa Shule Sista Basila Materu amesema Shule hiyo inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa maktaba itakayowasaidia walimu kutoa mazoezi mengi kwa wanafunzi ili kuwajenga kitaaluma na kuweza kufaulu mitihani yao na kuendela na hatua nyingine za kitaaluma.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mwanaidi Ali Khamis akikata keki ya kuadhimisha jubilee ya miaka 25 ya Shule ya Sekondari Loreto iliyopo Nyakato Mkoani Mwanza Oktoba 29, 2023.

Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza Mwashamu Renatus Nkwande amewaasa wanafunzi wa Shule hiyo kuhakikisha elimu wanayoipata inawasaidia kutatua changamoto katika jamii na kusaidia kuinua jamii zao kuondokana na umasikini na utumwa wa fikra.

Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Mhe. Mwanaidi Ali Khamis akiendesha harambee ya ujenzi wa Maktaba ya Shule ya Sekondari Loreto iliyopo Nyakato Mkoani Mwanza wakati wa maadhimisho ya Jubilee ya miaka 25 ya Shule hiyo Oktoba 29, 2023.

By Jamhuri