Katika kuunga mkono juhudi za Serikali kuwainua vijana na wanawake kupitia mradi wa kuwawezesha kulima, kuvua na kufuga kibiashara (BBT), Benki ya NMB imetenga jumla ya Sh. bilioni 20 pamoja na kuwaelimisha vijana na wanawake hao namna ya kupata mikopo hiyo.

Pia NMB imetenga Sh. bilioni 20 kwa ajili ya ujenzi wa maghala ya kuhifadhi mazao ya wakulima nchi nzima, ambapo kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita jumla ya Sh.bilioni saba tayari zimeishatolewa.

Hayo yameelezwa na Meneja wa NMB Kanda ya Nyanda za Juu, Bw. Straton Chilongola alipokuwa akimweleza Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Majaliwa Kassim, alipotembelea banda la benki hiyo katika viwanja vya John Mwakalange jijini Mbeya, yanapofanyika maonesho ya Kimataifa ya Kilimo ya Nane Nane.

Chilongola amesema, pamoja na mambo mengine pia benki hiyo inatoa huduma ya mikopo ‘NMB Mshiko Fasta’ ambapo wakulima wanaweza kukopa kupitia simu za kiganjani hadi Sh. 500,000 kupitia simu za kiganja bila dhamana wala kufika kwenye matawi ya benki hiyo.

Alieleza kuwa, benki hiyo pia ni ya kwanza nchini kuwawezesha wakulima kupata mikopo kwa riba nafuu ya 9% kwa mwaka na malipo ni kulingana na muda wa mazao.

Waziri Mkuu ambaye alikuwa ameongozana na Waziri wa Kilimo, Mhe.Hussein Bashe na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mhe. Abdalah Ulega aliipongeza NMB kwa masuluhisho mbalimbali waliyonayo kwa wakulima,
na namna benki hiyo inatoa kipaumbele kwenye sekta ya kilimo ambayo ndio uti wa mgongo wa Taifa, na kuzidi kuinua pato la Mtanzania.

By Jamhuri