Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Chalinze

Kwa mujibu wa Taarifa za Sensa, ongezeko la idadi ya wanawake wanaotegemewa ndani ya familia imeongezeka kufikia asilimia 37.6, idadi ambayo inatoa fursa za kuwezesha wanawake katika jamii.

Kutokana na hilo Serikali imeendelea kufanya jitihada mbalimbali ikiwemo kurudisha mikopo ya asilimia 10, mfuko kusaidia wananchi kuendelea kutenga fedha kuwezesha wananchi kiuchumi na fursa nyinginezo.

Ridhiwani Kikwete, Mbunge wa Jimbo la Chalinze mkoani Pwani, aliyabainisha hayo kwenye uzinduzi wa Jukwaa la kuwezesha wanawake kiuchumi kata ya Kiwangwa, Tarafa ya Msata.

“Kupitia fursa mbalimbali zilizopo zikiwemo za
ndani ya Halmashauri na zile zinazosimamiwa na Serikali kuu wanawake wana nafasi ya kusaidia ukuaji wa kipato ndani ya jamii na familia” anaeleza Ridhiwani.

Ridhiwani alieleza, kupitia ofisi ya mbunge amechangia sh.milioni 4.6 kuwezesha vikundi kukopeshana.

Hata hivyo mbunge huyo alieleza, ataendelea kuvishika mkono,kwa kushirikiana na Jukwaa la wanawake pamoja na vikundi mbalimbali vya wanawake jimboni humo.

Ridhiwani alieleza, mwanamke akiwezeshwa anaweza,kwani Taifa limekuwa likishuhudia kundi la wanawake kwasasa likifanya makubwa, kuanzia ngazi ya familia na maamuzi na , uongozi.

“Niwasihi Umoja ni nguvu, endeleeni kujiunga katika umoja wenu,vikundi,majukwaa ili kuweza kupata misaada na mkopo kirahisi kuliko kujigawa ,mkiwa kwa umoja mtashirikiana na kujifunza mengi “alisisitiza Ridhiwani.

By Jamhuri