Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia,Mafia

Mkuu wa Wilaya ya Mafia, mkoani Pwani, Aziza Mangosongo , amethibitisha kukamatwa kwa Ostadh wa madrasa anaedaiwa kulawiti watoto zaidi ya kumi ambapo pia zipo kesi nyingine zinaendelea kuchunguzwa.

Aidha amesema, licha ya serikali kupambana kupiga vita vitendo vya ukatili dhidi ya watoto lakini bado baadhi ya wakazi wa kisiwa hicho, wameonekana kutia pamba masikio hali inayosababisha kuongezeka kwa vitendo hivyo.

Akizungumza kwa hisia kali kwenye mkutano wa hadhara kijiji cha Kilindoni, Kitongoji cha Msufini, Mangosongo ameeleza tangu aanze kuhudumia Taifa kwa mara ya kwanza amekutana na wilaya inayo ongoza kwa vitendo vya ulawiti kwa watoto wa kike na wa kiume,ubakaji na mimba kwa wanafunzi hali ambayo inatishia usalama kwa watoto.

Amewataka wazazi,jamii kushirikiana kuwalinda watoto wao.

Nae Zaynab Matitu Vullu, Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake ,Mkoa wa Pwani, amemuomba Mkuu wa Wilaya Mafia kuangalia vyema ushahidi wa vitendo hivyo na kuwachukulia hatua kali wanaobainika ili kuwa funzo.

Vullu amekemea vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia, ulawiti, ubakaji kwani vinatishia usalama wa watoto.