Na. Abel Paul, Jeshi la Polisi- Katesh Manyara

Jeshi la Polisi Kikosi cha kuzuia wizi wa Mifugo limewataka Wananchi wa Kata ya Endasak Wilaya Hanang Mkoa wa Manyara kuwataja watu wanaojihusisha na wizi wa Mifugo katika eneo hilo huku likiwataka kuwa mstari wa mbele kutoa Ushahidi pindi unapohitajika mahakamani.

Hatua hiyo imekuja mara baada ya Kamanda wa Kikosi cha Kuzuia wizi wa Mifugo nchini Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi SACP Simon Pasua wakati alipofika katika mnada wa Endasak uliopo katika Wilaya ya Hanang Mkoa wa Manyara ambapo alisikiliza kero za wananchi ambao wanafanya biashara ya mifugo mnadani hapo juu ya kwepo kwa changamoto ya baadhi ya wafanyabiashara wasiowaaminifu.

Kamanda Pasua amewambia wananchi wa Kata ya Katesh kutoa ushirikiano pindi mhalifu anapokamatwa na kufikishwa mahakamani ikiwa ni pamoja na kutoa ushahidi ambapo amewaomba wananchi kuwataja wale wote wanaohusika na wale wanaojihusisha na wizi wa mifugo Lateshi.

SACP Pasua amebainisha kuwa zipo haki za mlalamikaji na mtuhumiwa katika kesi za jinai ambapo amewaomba wananchi kutambua endapo watamuona mwananchi aliyetuhumiwa na kesi za wizi wa mifugo akiwa nje watambue amedhaminiwa kwa mujibu wa sheria, huku akitoamsisitizo kwa wananchi kutoa Ushahidi Mahakamani.

Nao baadhi wa wananchi wanaofanya Biashara ya Mifugo katika mnada wa Endasak licha ya kutoa malalamiko yao kuwepo kwa baadhi ya wanafanya biashara wasiofuata taratibu mnadani hapo wameahidi kuendelea kushirikiana na Jeshi la Polisi kutokomeza uhalifu mnadani hapo.

Mwenyekiti wa mnada wa Endasak Bw. Alfan Ally Iddi amebainisha kuwa elimu ya sheria itolewe zaidi kwa wananchi ili kuwajengea uweelewa wa kisheria juu ya dhamana kwa watuhumiwa ili kuondokana na Imani Potofu juu ya Jeshi la Polisi.

By Jamhuri