Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Arusha

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuwainua wanawake kiuchumi kwa kuweka msingi unaochochea mabadiliko yanayojielekeza kukua kiuchumi.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Dkt. Dorothy Gwajima wakati wa Maadhimisho ya Kimataifa ya Siku ya Mwanamke anayeishi Kijijini yaliyofanyika Oktoba 15, 2023 kwenye Kijiji cha Olevolosi, Kata ya Kimnyak, Wilaya ya Arumeru Mkoani Arusha.

Waziri Dkt. Gwajima ameelezea nia ya Rais Dkt. Samia kuwainua Wanawake kwa kutaja baadhi ya mambo yanayotekelezwa na kuwagusa wanawake kwa kurejea takwimu, ikiwemo mikopo ya Sh. bilioni 713.8 iliyotolewa Julai 2022 hadi Machi, 2023 ambapo, imezalisha ajira 3,122,104 huku wanawake wakiwa asilimia 52.

Aidha, amesema mikopo hiyo ilienda kwa wajasiriamali 2,203,838 ambapo wanawake ni asilimia56

Kwa upande wa kilimo ambako wanawake wengi ndiyo nguvu kazi Dkt Gwajima amesema, Serikali imewezesha Ruzuku kwenye mbolea ambapo sasa bei ni Shilingi 73,468 badala ya Shilingi 109,000 kwa mfuko wa kilo 50 kupitia wakala waliopitishwa na Serikali katika ngazi za vijiji kwa mwaka 2023.
Vilevile, Serikali Kupitia mfuko wa pembejeo wa Taifa imetoa mikopo ya pembejeo za kilimo, mifugo na uvuvi.

Kwa upande wa mwanamke na ardhi amesema idadi ya wanawake wanaomiliki ardhi imekuwa ikiongezeka ukilinganisha na awali ambapo kufikia 2021/22 jumla ya Hatimiliki za Kimila 1,171,884 zimetolewa huku wanawake wakiwa 406,915.

Kuhusu biashara ya mazao ya kilimo, Dkt Gwajima amewaasa Wanawake kufanya biashara kwa kuongeza mnyororo wa thamani kwenye mazao ya kilimo na pia, kuhakikisha bidhaa zina alama ya msimbomlia (barcode), vifungashio nadhifu na vyenye ubora ili kukidhi vigezo kwenye masoko makubwa ya ndani na nje ya Tanzania,

“Nimefurahi kuona sabuni kutoka kwenye zao la asali kwenye moja ya mabanda niliyotembelea yaani zao la asali limeongezwa thamani” Dkt. Gwajima.

Kuhusu masoko, Waziri Dkt. Gwajima amewaasa wanawake kutumia fursa ya kidijitali kwa kufungua maduka ya kidijitali ili kutangaza bidhaa zao, kwani idadi ya watu wanaoona bidhaa mtandaoni ni kubwa na kwa muda mfupi.

Waziri Dkt Gwajima, ametumia fursa hiyo kuhamasisha wanawake kujiunga na majukwaa ya uwezeshaji kiuchumi.

“Tunayo majukwaa ya uwezeshaji wanawake kiuchumi lakini wengi hawajajiunga hivyo, Maafisa Maendeleo hakikisheni mnatoa elimu ya kutosha kwa Wanawake, hususan wa kijijini,” amehimiza Waziri Dkt. Gwajima.

By Jamhuri