RC Dodoma ashauri kufuatilia nyenendo za wafungwa wanapomaliza vifungo

Na Mary Gwera,Mahakama,Dodoma

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,Rosemary Senyamule ametoa ushauri kwa Jeshi la Magereza nchini kuona namna bora ya kufuatilia nyenendo za wafungwa pindi wamalizapo muda wa vifungo vyao kwa kushirikiana na Halmashauri kupitia Maafisa Ustawi wa Jamii ili dhana ya marekebisho ya tabia kwa wafungwa iweze kuonekana kwa vitendo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jana Januari 26, 2023 jijini Dodoma mara baada ya kukagua Mabanda ya Maonesho ya Wiki ya Utoaji Elimu ya Sheria yanayofanyika katika Viwanja vya Nyerere ‘Square’ jijini humo, Mhe. Senyamule alisema kuwa, asilimia kubwa ya wafungwa wanaomaliza vifungo vyao bado wanaendelea na tabia zisizo na maadili ikiwemo kufanya uhalifu kama wizi na mengineyo.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule (kushoto) akiuliza swali kwa Majaji na Maafisa waliokuwa wakitoa huduma katika Banda la Chama cha Majaji Wanawake Tanzania (TAWJA).

“Nimepita katika banda la Magereza nimeona wanafanya kazi nzuri sana, na hususani wajibu wa marekebisho kwa wafunga, lakini naona mara nyingi baada ya wafungwa kumaliza vifungo vyao hawafuatiliwi nyenendo na hatimaye wengine kuendelea kufanya uhalifu kama wizi na kadhalika, hivyo, ni muhimu Magereza kuangalia namna bora ya kuendelea kufuatilia nyenendo za wafungwa hata baada ya kumaliza vifungo vyao.

“Ni muhimu Magereza kuangalia namna ya kushirikiana pamoja na Halmashauri na hususani Maafisa Ustawi wa jamii kuangalia namna bora ya kuwawezesha wananchi hao baada ya kumaliza vifungo ili waweze kuendelea na maisha yao,” amesema Mkuu huyo wa Mkoa.

Ameongeza kuwa,mkoa wake upo tayari kushirikiana na Magereza kwa kuwa mfano (sample area) ambayo itakuwa eneo kwa ajili ya kuwasaidia wafungwa hao wanaomaliza vifungo hata kwa kupewa mitaji na elimu zaidi kupitia Halmashauri na Maafisa Ustawi wa Jamii ili kuendelea na maisha yao bila uhalifu kwa kuwa asilimia kubwa ya wafungwa waliomaliza kutumikia vifungo vya huendelea na tabia za kihalifu.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule (kulia) akimsikiliza kwa makini Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania-Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Wanjah Hamza (katikatika) alipokuwa akitoa maelezo kuhusu Kituo hicho na Usuluhishi kwa ujumla. Kushoto ni Hakimu Mkazi anayehudumu katika Mahakama Kuu-Kituo cha Usuluhishi, Mhe. Mohamed Burhani.

Kwa upande mwingine,Senyamule ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kazi nzuri inayoendelea kufanya ikiwa ni pamoja na uboreshaji pamoja na mabadiliko katika utoaji wa huduma zake mbalimbali.

Kadhalika amepongeza mhimili huo kwa kuja na kauli mbiu inayohusu masuala ya Usuluhishi kwa kuwa njia hii inaleta mshikamano baina ya wananchi.

“Njia hii ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya usuluhishi itaongeza utoaji haki kwa njia ya mapatano na makubaliano na wananchi watapata muda wa kufanya shughuli nyingine zitakazowaingizia kipato, hivyo wito wangu kwa wananchi watembelee maonesho haya kupata elimu zaidi ya usuluhishi,” amesema mkuu huyo wa mkoa.

Miongoni mwa Mabanda aliyotembelea Senyamule ni pamoja na Mahakama Kuu ya Tanzania-Kituo cha Usuluhishi, Jeshi ya Magereza, Jeshi la Polisi, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ‘BRELA’, Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), Chama cha Majaji Wanawake Tanzania (TAWJA) na mengine.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule (kulia) akipata maelezo kutoka kwa Mwakilishi wa Banda la Jeshi la Magereza. Mhe. Senyamule ametembelea Mabanda mbalimbali yaliyopo kwenye Maonesho ya Wiki ya Utoaji Elimu ya Sheria kwa umma leo tarehe 26 Januari, 2023.

Maonesho haya ya Wiki ya Sheria yanaendelea kufanyika nchi nzima hadi tarehe 29 Januari, 2023 na kilele cha Siku ya Sheria nchini itakuwa tarehe 01 Februari, 2023 ambapo itafanyika Kitaifa jijini humo na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa Mgeni Rasmi.

Kauli mbiu ya Wiki na Siku ya Sheria kwa mwaka huu ni; Umuhimu wa Utatuzi wa Migogoro kwa Njia ya Usuluhishi Katika Kukuza Uchumi Endelevu: Wajibu wa Mahakama na Wadau.

Mhe. Senyamule akipata maelezo kutoka Banda la Jeshi la Polisi.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule akisaini kitabu cha wageni alipofika banda la Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kwa ajili ya kupata maelezo na elimu kuhusu mfuko huo.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mhe. Rosemary Senyamule akiwa katika banda la Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.