SlaaRipoti ya utafiti iliyokabidhiwa kwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) inayomtaja Dk. Willibrod Slaa, kama mwanasiasa mwenye mvuto miongoni mwa wapinzani anayestahili kuwania urais kupitia Ukawa, hatimaye imepatikana; JAMHURI linathibitisha.

Kutupwa kwa ripoti hiyo kunatajwa kuwa ndiyo chachu iliyomfanya Dk. Slaa aachane na shughuli zote za kisiasa ndani ya Chadema. RIPOTI YOTE IMECHAPISHWA UK. 15-20 katika toleo hili la JAMHURI.
Utafiti huo uliofanywa na taasisi ya Tanzania Development Initiative Programme (TADIP) ambayo ni mali ya Chadema, unaonyesha kuwa Dk. Slaa anaongoza dhidi ya Edward Lowassa.
Ilikabidhiwa kwa uongozi wa juu wa Chadema Julai 26, mwaka huu, lakini chama hicho hakitaki kuitoa hadharani.


 TADIP ni taasisi ya Chadema ambayo kazi yake kubwa ni    kufanya utafiti na kutoa ushauri wa kitaalamu kwa chama hicho. Ripoti iliyokabidhiwa wiki mbili zilizopita, ni matokeo ya utafiti uliofanywa Mei na Juni, mwaka huu.
Kumekuwapo sintofahamu kati ya Dk. Slaa na viongozi wenzake ndani ya Chadema na Ukawa kwa jumla, lakini habari za uhakika zinasema mwanasiasa huyo amejiondoa Chadema kama njia ya kuonyesha kutokubaliana na wenzake kwa kumruhusu Lowassa kukaribishwa na hatimaye kupata ridhaa ya kukiwakilisha chama hicho na Ukawa kwenye uchaguzi wa rais.
Uongozi ndani ya Chadema unajitahidi kukanusha taarifa hizo, lakini uchunguzi uliofanywa na JAMHURI na vyombo vingine vya habari umethibitisha pasi na shaka kuwa Dk. Slaa amejiondoa Chadema.
Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya TADIP, George Shumbusho, amekabidhi ripoti ya utafiti kwa Chadema baada ya kufanya utafiti/kura ya maoni katika mikoa minane ya Tanzania Bara, kata 113 na kuwafikia wapigakura 1,727.
“Utafiti huu ulilenga kujua utayari wa wananchi kushiriki uchaguzi wakati wa kupiga kura, wagombea urais na vyama vya siasa vinavyokubalika pamoja na vipaumbele vya wananchi,” amesema Shumbusho kwenye barua yake ya kukabidhi ripoti ya utafiti huo.     

Nafasi ya Urais 2015
Kwa mujibu wa utafiti, Dk. Slaa anaongoza kwa asilimia 24.6 huku akifuatiwa kwa ukaribu na Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa ambaye alipata asilimia 22.9. Wanasiasa wengine walionekana kukubalika katika nafasi ya urais ni Profesa Ibrahim Lipumba kwa asilimia 9.6, Benard Membe aliyepata asilimia 7.6 na Dk. John Magufuli ambaye anakubalika kwa asilimia 4.3 kwa mujibu wa utafiti huo.
Wanasiasa wengine waliobaki wakiwamo wengi wa waliokuwa wametangaza nia kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Kiongozi Mkuu wa chama kipya cha ACT walionekana kukubalika katika nafasi hiyo chini ya asilimia 3. Hata hivyo, kuna kundi la wananchi (asilimia 17) ambao hawakuwa wameonyesha kuwa tayari kumchagua kiongozi yeyote atakayewafaa.

“Pia, hali hii ya kukubalika inaweza ikaendelea kubadilika haswa ikizingatiwa kuwa utafiti huu ulifanyika kabla vyama havijafanya uteuzi rasmi wa wagombea. Kukubalika kwa wanasiasa katika nafasi ya urais kunaonyesha kutofautiana baina ya mikoa iliyohusishwa. Dk. Slaa na Lowasa ambao ndio wanasiasa wanaonekana kukubalika zaidi katika utafiti huu walikaribiana katika mikoa yote iliyohusishwa; isipokuwa walitoafutiana kidogo,” inasema ripoti hiyo.
Dk. Slaa analionekana kukubalika zaidi katika mikoa ya Mbeya na Kigoma; huku Lowassa akikubalika zaidi katika mikoa ya Arusha, Dar es Salaam na Singida. Profesa Ibrahim Lipumba na Membe walionekana kukubalika zaidi katika Mkoa wa Mtwara (mikoa ya Kusini) huku Profesa Mark Mwandosya akiwa anakubalika zaidi mkoani Mbeya. Dk. Magufuli anakubalika zaidi katika mkoa wa Mwanza ikilinganishwa na mikao mingine. Matokeo haya yanaashiria kwamba mgombea wa urais atapata kura kwa kuzingatia eneo anakotoka na nguvu ya chama katika baadhi ya maeneo (mikoa).
“Utafiti huu pia umegundua kuwa watu rika tofauti tofuati wana mitizamo tofuati kuhusu nani anakubalika nafasi ya urais. Dk. Slaa na Lowassa wanaonekana kukubalika miongoni mwa Watanzania wenye umri tofauti tofauti,” inasema ripoti.


Hata hivyo, Dk. Slaa anaonekana kukubalika zaidi miongoni mwa vijana wenye umri kati ya miaka 27 mpaka 33 na watu wenye umri wa kati (miaka 38 mpaka 45) pamoja na watu wazima wenye umri wa miaka 51 mpaka 56.
Vijana wadogo, kati ya umri wa miaka 15 mpaka 26 wanaonekana kumkubali zaidi Lowassa wakifuatiwa na wazee zaidi ya miaka 56 ambao hata hivyo si wengi. Mbali na wanasiasa hao wawili, Profesa Lipumba, Membe na Dk. Magufuli walionyesha kukubalika zaidi kwa watu wazima wenye umri wa miaka 50 na kuendelea.
“Kutokana na matokeo haya, Dk. Slaa na Lowassa ndio wanasiasa wanaokubalika na makundi ya kiumri yenye asilimia kubwa zaidi ya wapiga kura,” inasema ripoti.

Ufuasi/uanachama wa Siasa
Vyama vyenye uwakilishi mkubwa bungeni vya CCM, CHADEMA na CUF vilionekana kuwa na wafuasi/wanachama wengi ikilinganishwa na vyama vingine. CCM ikiongoza kwa kuwa na asilimia 31.3 ikifuatiwa kwa karibu na CHADEMA kikiwa na asilimia 28.2 na CUF ilikuwa na asilimia 6.6 ya wafuasi/wanachama.
Vyama vingine vina asilimia chini ya 5 ya wafuasi/wanachama kwa mujibu wa utafiti huu.
Hata hivyo, kuna kundi kubwa la wananchi- sawa na asilimia 30 ambao walikiri kutokuwa na ufuasi/uanachama wa chama chochote.
“Hii inamaanisha kuwa vyama vyote vinahitaji kura za wafuasi/wanachama wao na za Watanzania ambao hawana chama chochote ili wapate viongozi bora. Sambamba na hilo, matokeo haya yanaashiria kwamba vyama vya upinzani vitakuwa na nguvu zaidi ama sawa na chama tawala endapo vitaunganisha nguvu zake,” umesema utafiti huo.

Chama gani kinakubalika 2015?
Matokeo yanaonyesha kuwa asilimia 42 ya wananchi wangechagua CCM; huku asilimia 37.8 wangechagua CHADEMA; na asilimia 10.1 wangepigia kura CUF. Chama cha ACT kingepigiwa kura na asilimia 2.9 ya wananchi kikifuatiwa na NCCR-Mageuzi kwa asilimia 1.3; huku TLP na UDP vikiwa vya mwisho kwa asilimia 0.2 na 0.1.
“Kwa haya matokeo ni dhahiri kuwa umoja wa vyama vya upinzani (UKAWA) unaweza kupata ushindi ama kuleta upinzani mkubwa kwa chama tawala tofauti vile ambavyo kila chama kingeshiriki uchaguzi kwa kujitegemea. Sambamba na hilo, wananchi wengi walioonyesha kutokuwa na ufuasi wa chama chochote wana uwezekano wa kupigia kura vyama vitatu ambavyo ni CCM, CHADEMA na CUF,” imesema sehemu ya utafiti huo.

Chama kitakachochaguliwa 2015
Wanachi walioshiriki katika utafiti wametoa sababu mbalimbali juu ya nini kitawasukuma kuchagua chama cha siasa.
Asilimia 27.7 wamesema wangechagua chama cha siasi kutokana na uongozi bora na sera makini, aslimia
18 walisema wangechagua chama kutokana na uwezo wake wa kuboresha maendeleo ya nchi. Wengine asilimia 14.3 walionyesha kuwa tayari kuchagua chama kutokana na uwezo wake wa kuleta mabadiliko kiuongozi na kiuchumi huku asilimia 10.8 wakioonekana kuchagua chama kutokana na kwamba kimekuwa madarakani tangu ukoloni, hawa ni wale ambao wangechagua chama tawala. Wanachi wengine walitoa sababu mbalimbali ambazo zinahusiana na uongozi bora, maendeleo na amani ya nchi.
“Matokeo haya yanadhihirisha kuwa wananchi watachagua chama kutokana namna kitakavyojinadi kushughulikia masuala ya maendeleo na uongozi bora. Hata hivyo, wapo wananchi ambao huenda wakapiga kura kutokana na mazoea ya chama tawala,” umesema utafiti.

Sababu za kuchagua chama
Kukubalika kwa vyama kunaonekana kuwa na tofauti mikoa mbalimbali. CCM iliongoza kwa kukubalika katika mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Mwanza na Singida. CHADEMA inakubalika zaidi katika mkoa wa Mbeya na kukaribiana na CCM katika mikoa mingine saba iliyohusika katika utafiti huo. Chama cha CUF kinaonekana kukubalika zaidi katika mkoa wa Mtwara huku ACT wakionekana kukubalika japo kwa kiasi kidogo katika mikoa ya Singida na Kigoma.

Kukubalika kwa chama kimikoa
“Kwa upande wa makundi rika, CCM inaoneka kukubalika zaidi kwa watu wenye umri wa utu uzima kuanzia miaka 45 na kuendelea huku CHADEMA kikionekana kukubalika zaidi miongoni mwa vijana na watu wenye umri wa kati. Kwa maneno meingine, CHADEMA itapigiwa kura zaidi na watu wenye umri chini ya miaka 45. CUF pia inakubalika zaidi kwa wazee wenye umri zaidi ya miaka 50. Hata hivyo, watu wenye mkubwa kwa mujibu wa sensa na kwa kujibu wa utafiti huu ni wachache chini ya asilimia 5,” utafiti umebaini.
Matokeo yanaonyesha kuwa CCM inakubalika zaidi kwa watu ambao hawana kiwango chochote cha elimu, na watu wenye elimu stashahada huku ikiwa imekabana koo na CHADEMA kwa kukubalika na watu wenye elimu ya msingi, sekondari na shahada ya kwanza. Vyama vya upinzani- CHADEMA, CUF na NCCR-Mageuzi vinaonekana kukubalika zaidi kwa watu wenye elimu ya juu, hasa shahada ya uzamili na shahada ya kwanza na kukubalika kwa kiasi kidogo miongoni mwa watu ambao hawana kiwango chochote cha elimu.
Utafiti unaonyesha kuwa makundi ya watu ambao hawajasoma na kundi la watu wenye elimu ya juu zaidi (shahada ya uzamili) yalikuwa na uwakilishi mdogo katika utafiti huo. Wengi wa wapigakura mwaka 2015 watakuwa na elimu ya msingi, sekondari na shahada ya kwanza.

Elimu na kukubalika kwa vyama
Mbali na makundi ya kielimu, utafiti huu pia umegundua kuwapo kwa tofuti juu ya kukubalika kwa vyama baina ya wanawake na wanaume. CCM ilionekana kukubalika zaidi kwa wanawake kuliko wanaume; huku chama wa CHADEMA kikionekana kukubalika zaidi wa wanaume. Vyama vya CUF na NCCR-Mageuzi viilikuwa na takribani asilimia sawa za kukubalika baina ya wanaume na wanawake.

Hitimisho na Mapendekezo
“Utafiti huu unaonyesha kuwa wananchi watakaoshiriki Uchaguzi Mkuu mwaka 2015 wengi wao watakuwa na umri wa ujana na umri wa kati (miaka 18 mpaka 40). Wengi wa wapigakura watakuwa na elimu ya msingi na sekondari na pia wengi watakuwa ni watu wanaojihusisha na kilimo, biashara na ujasiriamali. Kuna uwezekano pia wanaume wakawa na ushiriki mkubwa katika uchaguzi huu ikilinganishwa na wanawake.
“Asilimia kubwa ya wanachi wana utayari wa kupiga kura na asilimia ndogo wanaonekana kutokuwa tayari. Hata hivyo, ushiriki wa wapiga kura unaweza ukaathiriwa na sheria, kanuni, taratibu na taasisi zenye jukumu la usimamizi wa uchaguzi.
“Wanasiasa wakongwe watatu yaani Dk. Wilbroad Slaa, Edward Lowassa na Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF ndio wanasiasa ambao wanakubalika zaidi katika nafasi ya urais. Hata hivyo, kuna uwezekanao kwa mitizamo ya wananchi juu ya nani anakubalika urais kwa kuwa utafiti huu ulifanywa kabla uteuzi rasmi wa wagombea haujafanywa na vyama vya siasa.
“CCM inaonekana kukubalika zaidi ya vyama vingine ikifuatiwa karibu na CHADEMA ambacho kinafuatiwa kwa mbali na vyama vingine vya upinzani vya CUF, ACT na NCCR-Mageuzi. Kwa mantiki hiyo, muugano wa vyama vya siasa vya upinzani ndio njia kuu kwa kuimarisha nguvu ya vyama hivyo na kuviwezesha kupata ushindi mwembamba ama kuleta upinzani mkubwa.
“Mbali na mambo ya wagombea na vyama vya siasa, wapigakura wangependa serikali ijayo iboreshe hali ya huduma za kijamii ikiwamo elimu, afya, na maji. Kujenga uchumi imara utakaoboresha sekta za kilimo na viwanda ili kuleta tija katika utoaji wa ajira. Wapigakura wangependa kuona serikali itakayosimamia rasilimali za umma na kuwekeza katika mapambano dhidi ya rushwa,” utafiti umebaini.

Mapendekezo kwa Vyama vya UKAWA
Taasisi ya TADEP imetoa mapendekezo yafuatayo kwa Chadema na Ukawa kama kweli wanataka kuishinda CCM. Mapendekezo hayo ni:
• Vyama viendelee kuwahamasisha wananchi kuendelea kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapigakura. Elimu juu ya sheria na kanuni za uchaguzi iendelee kutolewa ili kuwafanya wananchi wawe na ufahamu wa kutosha wasije wakanyimwa kupiga kura kutokana na wasimamizi wenye maslahi na chama tawala.
• Dk. Slaa ni mwanasiasa ambaye anakubalika zaidi kusimamishwa na UKAWA katika kiti cha urais ikizingatiwa kuwa Lowassa amekoswa kuteuliwa CCM katika kinyang’anyiro hicho. Pamoja na Mgombea Mweza kutoka CUF, viongozi wa CUF na NCCR- Mageuzi watamwongezea hamasa Dk. Slaa kwakushiriki katika kampeni za kumnadi.
•Ikiwa vyama vya UKAWA vitaendelea na ushirikiano wake wakati wote wa uchaguzi, kuna uwezekano kwa wapinzani kushinda uchaguzi mkuu japo kwa asilimia ndogo.
•Kwa kuwa bado kuna wananchi wanaonekana kutokuwa na ufuasi wa chama, kwa kuwa utafiti huu unadhihirisha kuwa watu watapiga kura kwa itikadi za kisiasa, ni muhimu vyama vya UKAWA vikaendelea na jitihada za kuingiza wananchama wengi zaidi katika vyama vyao.
•Mikakati UKAWA ni muhimu ikalenga kuwafikia watu wenye elimu ndogo/uelewa wa kawaida, watu wazima na wazee, pamoja na akina mama.
Vipaumbele vya wagombea na ilani za vyama vinavyounda UKAWA zinapaswa zizingatie vipaumbele vya wananchi ikiwa ni pamoja na umuhimu wa kuboresha huduma za kijamii za elimu, afya, upatikanaji wa maji safi na salama. Ilani zizungumzie mipango ya kujenga uchumi imara utakaojikita katika sekta za kilimo na viwanda. Mbali na hayo, wananchi wangependa kuona serikali itakayosimamia vyema rasilimali za taifa kwa kupambana na rushwa, hivyo ni muhimu ilani za vyama washirika wa UKAWA kuzunguzia mambo haya.

 

By Jamhuri