Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Dodoma

Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa amesema kuwa safari ya treni ya mwendokasi ( SGR) kutoka Dar es Salaam mpaka Dodoma inatarajiwa kuanza Julai 25, 2024.

Mbarawa amesema hayo baada ya kufanya ziara ya kukagua miundombinu ya Reli ya Kisasa SGR, kipande cha Dar es Salaam na kujiridhisha kuwa treni hiyo itaanza kwa kuwa maandalizi yanaendelea vizuri.

“ Nimekagua miundombinu ya madaraja na vivuko pamoja na treni, kazi inakwenda vizuri na julai 25,2024 tunatarajia kuanza safari ya Dar es Salaam mpaka Dodoma,” amesema Waziri  Mbarawa.

Pia Waziri Mbarawa amesema kuwa nauli ya treni hiyo itakuwa fafiki kwa kila Mtanzania ataweza kusafairi kuanzia daraja la kwanza mpaka daraja la tatu

Amesema kuhakikisha safari ya treni hiyo inaanza bila kuwepo changamoto , kuanzia mwezi Juni treni hiyo itaanza safari ya Dar es Salaam mpaka Morogoro na mifumo ya tiketi itakuwa tayari na kutoa wito kwa Watanzania kuanza kusafiri kwa treni hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa amesema vivuko vya magari na vya kutembea kwa miguu vitakamailika mapema mwezi ujao na wataongeza vivuko vingine vya watembea kwa miguu pale itakapohitajika.

By Jamhuri