Serikali imesema kuwa mwaka ujao wa fedha itaajiri watumishi wa afya 10,112 ili kukabiliana na upungufu wa watumishi hasa maeneo ya vijijini.

Hayo yameelezwa bungeni, Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa anayeshughulikia Afya Dkt. Festo Dugange wakati akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, Khadija Taya aliyetaka kujua ni lini Serikali itashughulikia tatizo la upungufu wa watumishi kwenye vituo vya afya na zahanati nchini.

Amesema Serikali imeendelea kuajiri wataalamu wa kada mbalimbali za afya ambapo katika kipindi cha miaka mitatu (2021, 2022 na 2023), imeajiri watumishi 18,418 wa kada mbalimbali za afya na kuwapangia vituo kote nchini.