●COP 12 kufanyika Dar es Salaam Oktoba 6-9
Na Mwandishi Wetu
Tanzania imechaguliwa kuwa mwenyeji wa Mkutano wa 12 wa Nchi Wanachama wa Mkataba wa Nairobi (COP12), utakaofanyika kuanzia tarehe 6 hadi 9 Oktoba 2026.
Mkutano huo utafanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere (JNICC), jijini Dar es Salaam.
Mkutano huo unaiweka Tanzania katika ramani ya dunia kama kinara wa uhifadhi wa mazingira ya bahari na ukanda wa pwani na pia unafungua ukurasa mpya wa fursa za kiuchumi, uwekezaji, utalii na maendeleo ya Uchumi wa Buluu ambao umepewa kipaumbele katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Taarifa hiyo ilitolewa jana jijini Tanga na Naibu Waziri wa Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Reuben Nhamanilo Kwagilwa.
Alisema uenyeji wa mkutano huo ni matokeo ya imani kubwa ambayo jumuiya ya kimataifa imeiweka kwa Tanzania kutokana na uongozi wake madhubuti katika uhifadhi na usimamizi endelevu wa mazingira ya bahari.
Alisema kuchaguliwa kwa Tanzania kuwa mwenyeji wa COP12 kunakuja baada ya nchi kupewa pia nafasi ya kuongoza Kamati Tendaji ya Mkataba wa Nairobi katika mkutano wa COP11 uliofanyika Madagascar mwaka 2024.
Alisema hatua hiyo inaonyesha wazi kuwa Tanzania imeendelea kujijengea heshima kama taifa linaloongoza juhudi za kulinda Bahari ya Hindi, rasilimali zake na mifumo ya ikolojia inayotegemewa na mamilioni ya watu katika ukanda wa Afrika Mashariki na Bahari ya Hindi.








