Na Mwandishi Wetu

Wawakilishi wa Tanzania kwenye michezo ya Dunia kwa watu wenye ulemavu wa akili wameondoka kuelekea Ujerumani kushiriki michezo hiyo itakayoanza Juni 17 hadi 26.

Msafara huo wa watu 27 umeondoka saa moja asubuhi ya leo, wakipanda ndege ya Shirika la Turkish, ukiwa na matumaini makubwa ya kurejea na medali na zawadi nyingine nyingi katika mashindano hayo.

Kwa mujibu wa kocha mkuu wa timu hiyo, Deogratius Mdemu kikosi chake kilichoweka kambi ya wiki mbili jijini Arusha kina ari ya kufanya vizuri  na kubeba medali za dhahabu katika michezo ya riadha na mpira wa Wavu.

Mdemu alisema Watanzania wawaombee dua njema ili wafanye vizuri katika michezo hiyo ya Dunia.

Naye Matron wa wachezaji hao Saada Hamad Ali ameiomba Serikali kuwapokea kwa shangwe zaidi pindi watakaporejea kutoka Ujerumani na ushindi wa aina yake.

Amesema mara nyingi kwenye michezo ya Kimataifa, Tanzania hufanya vizuri ambako mwaka 2019, kwenye michezo ya Dunia iliyofanyika Abu Dhabi Falme za Kiarabu, Tanzania walikuwa mabingwa wa mpira wa wavu.

Aidha hivi karibuni Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo Dk Pindi Chana wakati anaikabidhi bendera ya Taifa timu hiyo alisema Serikali imedhamiria Tanzania kufanya vizuri kwenye michezo ya Kimataifa.

Chana alisema hiyo inaendana na miaka miwili ya Rais Samia Suluhu Hassan tumeshuhudia timu za Simba na Yanga zikifanya vizuri kwenye michezo ya Klabu bingwa Afrika na Shirikisho.

Kama hiyo haitisho timu ya Walemavu wa viungo ya Tembo Worries iliyoshiriki mashindano ya Dunia nchini Uturuki na timu ya Taifa ya wasichana ‘Serengeti girls’ iliyoshiriki Kombe la Dunia nchini India.

Waziri Chana alisema katika michezo hiyo ya Dunia nchini Ujerumani itashuhudiwa na Rais wa Zanzibar Dk Hussein Ali Mwinyi sambamba na Mawaziri wenye dhamana ya michezo bara na Zanzibar.

Msafara huo ulioelekea Ujerumani unaongozwa na makocha watatu akiwemo, Mdemu, Stephen Oloo na Agustino Shamte huku viongozi wengine ni Mkuu wa msafara ni Dk Mwanandi Mwankemwa, Mwakilishi wa wazazi Shamsa Diwani.

Wachezaji watakaoipambania nchi ni Sheha Hamad, Abdulrahmani Shabani (Kigamboni), Neverson Minja (Arusha), Herith Suleimani (Kiongozi wa wachezaji), Nassor Juma (Zanzibar) na Mathias Makanyaga (Geita).

Wengine ni Luqman Sabri (Temeke), Duncan Lucian na Ibrahim Mabeche (Kigamboni) na Oswald Kipoto (Kinondoni).

Kwa upande wa wasichana ni Fatuma Omari (Kigamboni), Shakira Omari na Johari Mohamed (Temeke), Rebeka Chales, Elizabeth Simon na Aziza Mussa (Arusha), Dorcas Julius na Sarah Kagoma (Kinondoni), Recho William (Tanga) na Maimuna Juma (Zanzibar).

By Jamhuri