Na Mwandishi Wetu,JamhuriMedia

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), Dkt. Ladislaus Chang’a, ambaye pia ni Afisa Kiungo wa Tanzania katika Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi (Intergovernmental Panel on Climate Change – IPCC) ameongoza vikao vya kamati ya jopo hilo (Contact Group) katika mkutano wa 58 wa IPCC (Fifty-Eighth Session of the Intergovernmental Panel on Climate Change – IPCC 58), uliofanyika Interlaken, Uswisi kuanzia Machi 13 hadi 18, 2023.

Jopo la IPCC lilikutana kwa lengo kuu la kuidhinisha Taarifa ya Sita ya Tathmini ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi “IPCC Synthesis Report of the Sixth Assessment cycle (AR6) – Climate Change 2023″.

Utaratibu wa kuidhinisha taarifa za tathmini za IPCC uhusisha kamati ambazo huteuliwa kufanya mapitio ya maeneo maalumu katika rasimu ya taarifa na kutoa mapendekezo.

Kwa upande wake, Dkt. Chang’a, aliteuliwa kuongoza kamati ya kuidhinisha “Sehemu A” ya taarifa hiyo (Section A and Figures, Summary for Policymakers of the Working Group III Contribution to the IPCC Sixth Assessment Report –SPM 1 and the associated Figure Caption) akishirikiana na Bi. Tina Christensen kutoka Denmark.

Sambamba na kuongoza kamati hiyo, Dkt. Chang’a alitoa mchango wa kitaalamu wa sayansi a mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi kwa Tanzania katika taarifa hiyo kwa manufaa ya nchi yetu na hivyo kuitangaza vyema Tanzania Kimataifa.

Katika hatua nyingine, Dkt. Chang’a alikutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Taasisi ya Hali ya Hewa ya Korea (Korean Meteorological Adminstration – KMA) kuhusu ushirikiano na TMA katika masuala ya hali ya hewa ambapo kiongozi huyo alisema KMA iko tayari kupanua wigo wa ushirikiano na TMA.

Miongoni mwa maeneo ambayo walikubaliana KMA na TMA kushirikiana ni matumizi ya mifumo ya kiditajitali katika uandaaji wa utabiri wa hali ya hewa,ufungashaji na usambazaji wa taarifa za hali ya hewa.

Aidha, Dkt. Chang’a alikutana na kufanya mazungumzo na Shirley Matheson ambaye ni Mratibu wa masuala ya mabadiliko ya tabianchi katika Shirika la Uhifadhi wa Mazingira (Worldwide Fund for Nature –WWF) na kujadiliana kuhusu WWF kushirikiana na TMA katika masuala ya hali ya hewa na tabianchi.

IPCC ni Jopo la Kimataifa la Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi liloanzishwa na Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) na Programu ya Mazingira ya Umoja wa Mataifa (United Nations Environmental Programme – UNEP).

Jopo hilo linaundwa na nchi zote wanachama wa WMO kupitia wataalamu ambao ni Maafisa Viungo (Focal Points) wanaowakilisha nchi zao katika Jopo hilo.

Kwa Upande wa Tanzania, TMA imepewa dhamana ya kuiwakilisha Tanzania katika masuala hayo ambapo Afisa Kiungo wa Tanzania ni Dkt.Ladislaus Chang’a.

Jukumu la Msingi la IPCC ni kutumia tafiti mbalimbali zinazohusu Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi na kuandaa taarifa za Tathmini (Synthesis Reports) ambazo ni muhimu katika kutoa maamuzi ya sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi.

Tangu Jopo hilo lianzishwe mwaka 1988 limefanikiwa kutoa Taarifa tano (5) za tathmini.

By Jamhuri