Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Rufiji

Mamlaka ya Dawa na vifaa Tiba Tanzania (TMDA) imetoa elimu ya namna ya kutumia dawa kwa usahihi na kuepuka matumizi holela ya dawa, ikiwemo kutotumia dawa zinazoweza kuzuia kupata ujauzito kwa wanafunzi na dawa zinazoongeza nguvu za kiume hali itakayoweza kusababisha migogoro katika ndoa.

Akizungumza na Wanafunzi, Mkaguzi wa dawa TMDA ,Jafari Saidi katika Shule ya Sekondari Bwawani Mjini, kata ya Umwe Wilayani Rufiji mkoani Pwani , amewataka Wanafunzi kuripoti kutoa taarifa mapema pindi waonapo Madhara yatokanayo na matumizi ya dawa.

“Tumewafundisha wanafunzi madhara ya kabla na baada ya matumizi ya dawa, dawa inaweza kusababisha ukababuka, kuvimba au ukawa husikii ukawa mtu huwezi kuona” amesema Saidi.

“Watu wanakaa kwenye ndoa miaka kumi,  wanamaliza waganga wakienyeji tatizo mtoto hapatikani, kumbe wakati huo  ulikuwa unatumia hizi dawa kama pipi.

” Hizi dawa zinachangamoto nyingi, zimeshaua wengi hamruhusiwi kutumia” alisisitiza Saidi.

Anasema amesema kuwa zoezi la utoaji wa elimu litaendelea kwa muda wa wiki moja ambapo watazungumza na wanafunzi katika Shule mbalimbali kutoa elimu ya matumizi sahihi ya dawa.

Kwa upande wake Kaimu Afisa elimu sekondari Florine Bwikizo amemuomba Mkurugenzi wa TMDA kuwawezesha wafanyakazi  wa Taasisi hiyo kutoa elimu  katika shule za awali na msingi ili elimu hiyo ifike kwa jamii nzima.

Akizungumza baada ya semina hiyo Mwalimu wa afya wa shule ya Sekondari Bwawani Mjini Justina Mnyeta ,alisema semina hiyo imewasaidia Wanafunzi pamoja na Walimu kujua matumizi ya dawa na namna ya kumuhudumia Mgonjwa.

“Changamoto tulizokuwa nazo ni Wanafunzi kutumia dawa kwa mazoea ya kawaida, mfano dawa imeandikwa kutwa mara tatu  yeye utakuta anakunywa saa 1 alafu saa 7 badala ya kupisha masaa nanenane” anasema Mnyeta.

Kwa upande wa wanafunzi wa shule hiyo akiwemo Shani Mpita alisema semina imemsaidia namna ya kugundua dawa ina madhara au haina madhara.

By Jamhuri