N .Abel Paul wa Jeshi la Polisi

Vikundi vya ulinzi shirikishi katika Jiji la Arusha vimewezeshwa vifaa vya mawasiliano kwa lengo la kurahisisha mawasiliano wakati wakiimarisha ulinzi katika mitaa mbalimbali ya Jiji la Arusha.

Akikabidhi vifaa hivyo ambavyo ni simu za mkononi kwa vikundi vya ulinzi vilivyotolewa na kampuni ya Vodacom Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini Mrisho Gambo leo Novemba 17, 2022 amesema vitasaidia katika kuimarisha ulinzi na usalama katika Jiji la Arusha ambalo ni kitovu cha utalii hapa nchini.

Aidha mbunge huyo ameishukuru Kampuni ya Vodacom kwa kuunga juhudi za ulinzi na usalama katika Jiji la Arusha ambapo amesema msaada huo utakua chachu ya kudhibiti uhalifu katika jiji hilo, pia ametoa wito kwa wananchi kuendelea ushirikiano kwa Jeshi la polisi na vikundi vya ulinzi shirikishi.

Naye Mwakilishi wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha ambaye pia ni Afisa mnadhimu ACP Mary Kipesha amesema kuwa lengo la Polisi ni kuwa na ushirikiano na jamii kiutendaji, kusogeza huduma za usalama kwa wananchi, lakini pia kuinua uchumi wa wao kwa kuhakikisha wanakua salama katika shughuli zao.

Kwa upande wa Meneja wa Vodacom kanda ya Kaskazini Bwana George Venant amesema kampuni hiyo inayofuraha kushirikiana na Jamii katika suala zima la ulinzi ambapo amesema zitasaidia katika kuimarisha hali ya usalama katika mitaa mbalimbali.

Akitoa shukrani kwa niaba ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha, Mkuu wa Polisi Wilaya ya Arusha Mjini Mrakibu Mwandamizi wa Polisi SSP Edith Swebe ametoa wito kwa vikundi vya ulinzi shirikishi vilivyokabidhiwa vifaa hivyo kuhakikisha wanavitumia katika malengo yaliyokusudiwa ya ulinzi.

By Jamhuri