Na Samwel Mtuwa – Geita

Imeelezwa kuwa Viwanda vya Uchenjuaji Madini Mkoani Geita vimeongeza tija katika biashara ya madini nchini ambapo kiasi cha Shilingi bilioni 3.2 hukusanywa kila mwezi kupitia vituo hivyo.

Hayo yamebainishwa Novemba 12 , 2023 na Waziri wa Madini Anthony Mavunde wakati akizindua Ofisi ya kampuni ya Jema Afrika ambayo inajihusisha na shuguli za uchenjuaji madini ya dhahabu mkoani Geita.

Mavunde amefafanua kuwa Serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa wawekezaji wote katika mnyororo mzima wa sekta ya madini nchini ikiwa pamoja na kuweka mazingira mazuri na salama yenye lengo la kufanya uwekezaji ulio na tija kwa Taifa na jamii kwa ujumla.

Akielezea kuhusu mikakati iliyopo chini ya Serikali ya awamu ya sita, Waziri Mavunde ameleeza kuwa kwasasa kuna mikakati mbalimbali ya mageuzi hususani kwa wachimbaji wadogo kwa kufanya utafiti wa kina utakao toa taarifa sahihi za aina ya miamba na madini iliyopo ili kuchimba bila kubahatisha.

Aidha, Waziri Mavunde aliongeza kuwa uchumi wa sasa ni shirikishi hivyo Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wote ili kufungamanisha sekta zinazotegemeana kiuchumi kama Vision 2030 inavyosema kuwa Madini ni Maisha na Utajiri.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Geita Martine Shigela ameipongeza kampuni ya Jema Afrika kwa kushirikiana na Serikali katika kutanua wigo wa sekta ya madini ndani ya mkoa wa Geita.

Kwa upande, wake Mkurugenzi Mtedaji wa Jema Afrika Jumanne Mokili ameishukuru serikali kwa kuweka Sera rafiki kwa wawekezaji ikiwa pamoja kuimarisha miundombinu mbalimbali.

Mpaka sasa Mkoa wa Geita una viwanda zaidi 60 vya uchenjuaji madini ya dhahabu katika maeneo ya Nyarugusu , Lwamgasa, Magenge, Kaseme ,Geita na Butobela.

By Jamhuri