Waziri Mavunde akutana na Kampuni ya MAST na AKMENITE

Viwanda vya Uchenjuaji madini kujengwa Ruvuma, Dodoma, Katavi na Lindi

Ujenzi wa viwanda kuanza mapema mwaka huu

Waziri wa Madini Mhe. Anthony Mavunde amekutana na kufanya mazungumzo wadau wa Sekta ya Madini kutoka Kampuni ya Mineral Access System Limited(MAST) ikiwakilishwa na Mkurugenzi wa Kampuni hiyo Bw. Georgefrey Kente pamoja na Mwekezaji toka Lithuania, Bw. Arunas Sermuksnis; Mkurugenzi wa kampuni ya Akmenite Limited ambao wote wameonesha nia kuanzisha ujenzi wa viwanda vya uchenjuaji wa madini ya metali kuunga mkono jitihada za serikali za kuongeza thamani madini nchini.

Akizungumza katika mkutano huo, Mkurugenzi wa Kampuni ya MAST Bw.Georgefrey Kente ameonesha utayari wa kampuni yake kujenga viwanda vitatu vya uchenjuaji wa madini ya metali katika mikoa ya Ruvuma,Dodoma na Lindi ambapo ujenzi wake unatarajiwa kuanza mapema mwaka huu ambapo jumla ya zaidi Dola za kimarekani 15m USD zitatumika kukamilisha ujenzi huo.

Naye, Bw. Arunas Sermuksnis Mkurugenzi wa kampuni ya Akmenite Limited naye amehakikishia Serikali kwamba wataleta nchini teknolojia ya kisasa ya uchenjuaji wa metali ili shughuli za uongezaji madini kufanyika ndani ya nchi na hatua za awali za uanzishwaji wa kiwanda hicho zimeanza tayari.

Kwa upande wake, Waziri wa Madini Mhe Anthony Mavunde amezipongeza Kampuni hizo kwa uamuzi huo wa kuwekeza viwanda vya uchenjuaji madini ndani ya nchi na kuhimiza ukamilishaji wake uwe ndani ya muda mfupi ili wachimbaji wa Tanzania wanufaike na fursa hiyo kwakuwa kwa hivi sasa moja ya changamoto kubwa inayowakabili wachimbaji wa madini ya metali ni kukosekana kwa teknolojia ya uchenjuaji ili kutosafirisha madini ghafi nje ya nchi.

Pia, Waziri Mavunde amewahakikishia wawekezaji hao kwamba Serikali kupitia Wizara ya Madini itatoa ushirikiano wa kutosha na kuhakikisha uwekezaji huo unafanyika kwa manufaa ya maendeleo ya sekta ya madini Tanzania.

Aidha, wadau hao wameishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Hassan kwa kuweka mazingira rafiki ya uwekezaji na kuwajali wachimbaji wadogo.

By Jamhuri