Na Mwamvua Mwinyi, JamhuriMedia, Kibaha

WAZAZI na walezi Mkoani Pwani wameaswa kujenga ukaribu kwa watoto wao pamoja na kuwapa haki ya kujieleza pale inapobidi ,ili waweze kufichua Yale ambayo yanawakabili hasa kwenye vitendo vya unyanyasaji wa watoto.

Aidha jamii imetakiwa kuhakikisha ulinzi na usalama wa mtoto kwa kumuondolea vikwazo na kutoa taarifa kwa wanaofanya vitendo vya ukatili ili mtoto aweze kutimiza ndoto zake.

Rai hiyo imetolewa na Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani ,Rashid Mchatta alipokuwa akizindua mradi wa Usalama wa Watoto (UWAWA) awamu ya pili unaosimamiwa na Christian Social Services Commission (CSSC),ulioanza 2023 septemba na utakamilika 2026.

Mchatta alieleza ,watoto wanakabiliwa na changamoto nyingi ambapo jamii inatakiwa kusema na watoto wao na kuwalinda pasipo kuwa wakali.

“Mradi huu wa UWAWA inaunga mkono juhudi za Serikali kuzingatia usalama na haki kwa watoto, lengo ni kuimarisha usalama wa watoto” alifafanua Mchatta.

Naye Ofisa elimu Mkoa wa Pwani Sara Mlaki aliwataka wazazi kusimamia malezi ya watoto na kufuatilia masomo yao bila kuwaachia walimu pekee.

Mlaki aliwataka wale wazazi wanaonyanyasa watoto wao waache na badala yake waongeze upendo kwao

Alisema, vitendo vya ukatili kwa watoto wakati mwingine vinatokana na utandawazi ambapo amewasihi wasitumie mitandao ya kijamii kuonyesha vitendo vya ukatili kwa watoto.

Kwa upande wake Meneja wa Kanda ya Mashariki wa (CSSC) Makoye Wangeleja aliushukuru mkoa kwa kutoa ushirikiano.

Alieleza,vita unyanyasaji na ukatili kwa watoto siyo lelemama ,watu wanaowafanyia vitendo hivyo ni watu ambao huwezi kuwafikiri na inabidi kujipanga ili kukabili vitendo hivyo .

Makoye alieleza, wazazi wamekuwa wakikosa muda wa kukaa na watoto ,wanaachia wadada wa kazi na walimu ,na wakirudi nyumbani wanashindwa kujenga urafiki na watoto na kuwa wakali hata wakitaka kuelezwa Jambo.

“Hili ni tatizo kubwa, unakuta mtoto anataka kujieleza,labda kaffanyiwa vitendo vya ukatili,mzazi anamnyamazisha mtoto, unakuta mtoto anayasema nje ya familia suala ambalo sio jema kwani wanakosa uhuru wa kuzungumza na kujieleza” alieleza Makoye.

Ofisa ustawi wa jamii Kibaha Mjini, Mary Michael alieleza chanzo kingine ni wazazi kutelekeza watoto huku wakijikuta wakikosa malezi mema.

Aliomba ushirikiano uwepo kwa ngazi za jamii, Serikali, madawati ya jinsia, Jamii na wadau ili kukomesha vitendo vya kijinsia kwa watoto.

By Jamhuri