WAZIRI MKUU Dkt. Mwigulu Nchemba ameondoka nchini leo (Jumatatu, Mei 25, 2026) kwenda Brazzaville, Jamhuri ya Kongo kumwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye Mkutano wa 61 wa Mwaka wa Bodi ya Magavana wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).
Mkutano huo utafanyika Mei 26 – 27, 2026, katika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Kintele jijini Brazzaville, Jamhuri ya Kongo.
Mkutano huu ni jukwaa muhimu la majadiliano ya kimkakati kuhusu masuala muhimu ya maendeleo ya dunia, yakihusisha nchi wanachama, taasisi za kikanda na kimataifa ambalo linahusisha kuhamasisha upatikanaji wa rasilimali za fedha ili kuwezesha utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya Afrika na kuimarisha uwezo wa bara kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiuchumi na kifedha duniani.
Mkutano huo utawakutanisha wajumbe wapatao 3000 ikiwemo Mawaziri wa Fedha na Magavana wa Benki Kuu za Afrika, Watunga Sera, wafanyabiashara, Taasisi za Kifedha, Washirika wa Maendeleo, Wajasiriamali pamoja na Wawekezaji.







