ZAMU YA SIMBA SC LEO KUONESHA MAKUCHA YAKE KWENYE MICHEZO YA KIMATAIFA

Kikosi cha Simba Sc

SIMBA SC inarejea kwenye michuano ya Afrika leo baada ya miaka minne, itakapomenyana na Gendarmerie Tnale ya Djibouti katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Kwanza Ligi ya Mabingwa Afrika Uwanbja wa Taifa jijini Dar es Salaam jioni ya leo.
Mara ya mwisho Simba SC kushiriki michuano ya Afrika ilikuwa mwaka 2012 na ikatolewa Raundi ya Kwanza tu na Recreativo do Libolo ya Angola kwa jumla ya mabao Simba 5-0, ikifungwa 1-0 Februari 17 Dar es Salaam na 4-0 ugenini  Machi 3.
Baada ya kukosekana kwa miaka minne, hatimaye timu yenye rekodi nzuri zaidi nchini kwenye michuano ya Afrika ikiwa ni pamoja na kufika fainali ya michuano hiyo mwaka 1993 enzi hizo ikijulikana kama Kombe la CAF kabla ya kuunganishwa na Kombe la Washindi kuwa Shirikisho  inarejea rasmi leo.

Mchezo dhidi ya Gendarmerie Tnale utachezeshwa na refa Alier Michael James atakayepuliza filimbi akisaidiwa na Abdallah Suleiman Gassim, Gasim Madir Dehiya washika vibendera, Kalisto Gumesi mezani na Kamishna Mmonwagotlhe Edwin Senai kutoka Botswana.
Mchezo wa marudiano utakaochezwa Djibouti kati ya Februari 20 na 21,2018 wenyewe utachezeshwa na waamuzi kutoka Burundi na Kamishna wa mchezo atatokea nchini Rwanda.
Mwamuzi wa kati ni Eric Manirakiza akisaidiwa na mwamuzi msaidizi namba moja Pascal Ndimunzigo, mwamuzi msaidizi namba mbili Willy Habimana,mwamuzi wa akiba Pacifique Ndabihawenimana na kamishna Gaspard Kayijuka.
Simba SC inaingia kwenye michuano ya Afrika ikiwa katika kiwango kizuri baada ya kucheza mechi 17 za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara bila kupoteza hata moja, ikiwa inaongoza kwa pointi zake 41, ikifuatiwa na mabingwa watetezi, Yanga wenye pointi 34 na Azam FC katika nafasi ya tatu kwa pointi zao 33.
Na ikiwa ni wastani wa mwezi mmoja tangu mabadiliko ya benchi la Ufundi, kocha Mfaransa Pierre Lechantre akichukua nafasi ya Mcameroon Joseph Marius Omog, Simba SC inatarajiwa kutuma salamu Afrika juu ya urejeo wake kwa ushindi mnono leo.
Lechantre anayesaidiwa na Mtunisia, Mohamed Aymen Hbibi, Mrundi Masoud Juma na mzalendo, Muharammi Mohammed ‘Shilton’ kocha wa makipa hatarajiwi kuwa na mabadiliko makubwa kutoka kikosi kilichocheza na Azam FC na kushinda 1-0 Jumatano.
Langoni anaweza kurudi ‘Tanzania One’, Aishi Manula atakayekuwa analindwa na mabeki Shomary Kapombe, Erasto Nyoni, Yussuph Mlipili na Asante Kwasi, viungo Jonas Mkude, Shiza Kichuya, Said Ndemla, James Kotei na washambuliaji kama kawaida John Bocco na Emmanuel Okwi.
Katika benchi kama kawaida watakuwapo Emmanuel Mseja, Muzamil Yassin, Mohammed Hussein ‘Tshabalala’, Mwinyi Kazimoto, Juuko Murshid, Laudit Mavugo, Jamal Mwambeleko, Nicholas Gyan na Ally Shomary.
Wawakilishi wengine wa Tanzania kwenye michuano hiyo, Zimamoto ya Zanzibar leo wanaikaribisha Wolaitta Dicha ya Ethiopia Uwanja wa Amaan, Zanzibar.
Ikumbukwe jana katika Ligi ya Mabingwa, wawakilishi wa Tanzania, Yanga SC walipata ushindi mwembamba wa 1-0 dhidi ya Saint Louis Suns United ya Shelisheli katika mchezo wa kwanza wa Raundi ya Kwanza Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, wakati JKU ya Zanzibar ililazimishwa sare ya 0-0 na Zesco Uwanja wa Amaan.