Na Mwandishi Wetu, JamhuriMedia, Arusha
Benki ya NMB imejipanga kupanua ufadhili kwa wafanyabiashara na wawekezaji ili kuongeza upatikanaji wa mitaji na kuharakisha utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayotegemea sekta binafsi kubeba sehemu kubwa ya uwekezaji unaohitajika kuifikisha Tanzania kwenye uchumi wa dola za Marekani trilioni moja ifikapo 2050.
Akizungumza na waandishi wa habari pembezoni mwa Kongamano la Kitaifa la Wanamipango jijini Arusha, Septemba 17, 2026, Mkurugenzi wa Mipango wa NMB, Francis Haraka Mittah, alisema matarajio ya sekta binafsi kuchangia takribani asilimia 70 ya mahitaji ya uwekezaji yanaipa sekta ya fedha jukumu kubwa la kuwezesha mitaji, kuanzia kwa wawekezaji wakubwa hadi wafanyabiashara wadogo.
Mittah alisema NMB inaendelea kubuni njia za kuongeza upatikanaji wa fedha, ikiwamo bidhaa zitakazowezesha wafanyabiashara wadogo wanaokidhi vigezo kupata mitaji kwa masharti yanayoendana na uwezo wao na kutumia njia nyingine za kutathmini uwezo wa mteja kulipa. Alisema biashara ndogo, zikiwamo za mama na baba lishe, zina nafasi muhimu katika kuzalisha ajira na kipato.
Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, amesisitiza umuhimu wa Serikali kujenga mfumo unaowezesha sekta binafsi badala ya kuielekezea nguvu kubwa kwenye udhibiti, akisema malengo ya Dira 2050 yatahitaji biashara kuongeza uzalishaji, uwekezaji na ajira. NMB imesema itaendelea kushirikiana na Serikali na wadau wengine kupanua ufadhili wa shughuli za kiuchumi zinazochangia utekelezaji wa Dira 2050.



